Waziri mkuu wa zamani wa Sudan, Sadiq al-Mahdi amefariki dunia kutokana na virusi vya corona.Mwanasiasa huyo amefariki dunia wakati akipatiwa matibabu katika nchi ya Umoja wa Falme za Kiarabu.

Mahdi aliyefariki akiwa na umri wa miaka 84, ndiye waziri mkuu wa mwisho wa Sudan kuchaguliwa kidemokrasia kabla ya kuondolewa madarakani mwaka 1989 kwa mapinduzi ya kijeshi yaliyomuingiza mamlakani rais wa zamani Omar al-Bashir.

Chama chake cha Umma chenye siasa za wastani, kilikuwa moja ya vyama vikubwa vya upinzani na Mahdi alisalia kuwa kiongozi mwenye ushawishi.