Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ametoa siku 4 kuanzia leo hadi kufikia Novemba 20, wakuu wa mikoa kupita kwenye viwanda na maghala ya saruji waangalie kwa nini bei ya bidhaa hiyo imepanda bila sababu ya msingi

Akizungumza mbele ya Rais John Magufuli baada ya kuapishwa kuwa Waziri Mkuu katika viwanja vya Ikulu, Chamwino jijini Dodoma, Waziri Majaliwa amehoji, sababu za bei ya saruji kupanda wakati Serikali haijapandisha kodi, makaa ya mawe wala kujafanya mabadiliko yoyote.

“Kuna upandaji wa saruji bila sababu za msingi, miaka mitano iliyopita tulijenga mazingira ya biashara kuwa rahisi. Hatukutarajia saruji kupanda, mheshimiwa rais (Rais Magufuli) naaanza na hilo.”

“Tarehe 20 saa nne asubuhi, maofisa wangu wanipe ripoti tujue kwanini saruji imepanda wakati serikali haijapandisha kodi, makaa ya mawe. Tunahitaji maelezo kwanini bei ya saruji imepanda kwa kiasi hicho,” amesema Majalia.

Aidha, Majaliwa amesema, kwa kuwa moja ya kazi yake kubwa ni kuhakikisha malengo ya Serikali na ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) 2020 – 2025 inatimia, atapita kila wizara kusisitiza hilo.


Pia, Waziri Majaliwa amewashukuru wabunge kwa kuridhia jina lake kuwa Waziri Mkuu akisema, tabia yake ni ile ile ya kuwasikiliza na kuwahudumia wabunge kwa maslahi ya Taifa.