Vyombo vya ulinzi na usalama mkoa wa Dar es salaam, vimefanikiwa kuwatia mbaroni wahamiaji haramu 36 raia wa Ethiopia na Somalia walioingia nchini kinyume na taratibu, ambapo mkuu wa mkoa huo Aboubakar Kunenge ametoa onyo kali kwa raia wa Tanzania, wanaoshiriki kuwafadhili na kuwasafirisha ili wapate fedha.

Kunenge amesema Wahamiaji hao walikamatwa usiku wa kuamkia November 15, 2020 kwenye fukwe za Mbweni ambapo kati yao, 30 wanatoka nchini Ethiopia na Sita wanatokea nchini Somalia.

Aidha Kunenge amesema hata utaratibu unaotumika kusafirisha watu hao unakiuka sheria, haki na utu wa binadamu sababu wengi wao wanafungiwa kwenye kontena zisizokuwa na hewa na pindi wanapobainika kufariki Dunia maiti zao hutupwa kwenye vichaka.

Pamoja na hayo RC Kunenge amevipongeza vyombo vya ulinzi na usalama kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya.

Kwa upande wake Afisa uhamiaji mkoa wa Dar Es Salaam, Kamishna Msaidizi Edmund Mrosso amesema kinachofuata baada ya wahamiaji hao kukamatwa watafikishwa mahakamani kwa kosa la Kuingia nchini kinyume na taratibu.

Aidha Kamishna Mroso amesema kwa wale wanaowasafirisha au kuwahifadhi wahamihaji hao, adhabu inaelekeza kifungo cha miaka 20, faini ya shilingi milioni 20 au vyote kwa pamoja ikiwa ni pamoja na kutaifisha mali zilizotumika.