Asteria Muhozya na Issa Mtuwa, Mirerani
Kwa mara nyingine tena Ukuta unaozunguka Migodi ya Tanzanite Mirerani wenye urefu wa kilomita 24.5 umeingia kwenye historia nyingine baada ya kufungwa jumla ya Kamera 306 za Usalama zenye uwezo wa kufanya kazi katika mazingira yoyote ikiwemo kumbaini mhalifu. 
Kamera hizo zimewekwa kufuatia kuwepo umuhimu wa eneo husika kufungwa mfumo wa CCTV kwa lengo la kugundua vitu na watu wanaoingia eneo la Ukuta, kuhifadhi taarifa za Kudumu, kuzuia wanaokusudia kufanya uhalifu na kufuatilia matukio yanayofanyika eneo la ukuta huo.
 
Hayo yalibainishwa Novemba 17, 2020 na Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini Prof. Simon Msanjila wakati wa Hafla fupi ya kukabidhi mfumo huo kwa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.
 
“Kamera hizi zina uwezo wa kurekodi matukio wakati wa usiku, mchana, wakati wa jua, Kwenye vumbi, wakati wa mvua na zina uwezo wa kumtambua mhalifu aliyekwishafanya uhalifu kwenye Ukuta,’’ alisema Prof. Msanjila.
 
Kufuatia kufungwa kwa mfumo huo, Prof. Msanjila aliwaasa Wafanyakazi wa Wizara ya Madini na Taasisi zilizo chini yake kuendelea kufanya kazi kwa bidii huku wakisisitiwa kuzingatia Kanuni na Maadili ya Utumishi wa Umma.
 
Aidha, alitumia fursa hiyo kutoa rai kwa wadau wote katika eneo tengefu la Mirerani kujiepusha na vitendo vya rushwa, utoroshaji wa Madini ama kukiuka Sheria, Kanuni, Taratibu na miongozo mbalimbali inayosimamia Sekta ya Madini na kuiwezesha  Serikali kufikia malengo yake na kuwapo kwa tija katika Uwekezaji mkubwa wa miundombinu uliofanyika hapa Mirerani.
 
Pia, kufuatia matokeo chanya ambayo yanaonekana katika sekta ya madini,Prof. Msanjila alimwakikishia  Rais John Magufuli na watanzania kuwa wizara yake kwa kushirikiana na wadau mbalimbali  ndani na nje  itahakikisha kuwa sekta hiyo inadhihirisha kuwa muhimu katika kujenga  wa nchi.
 
Akizungumzia mipango mingine iliyobaki kukamilishwa katika eneo hilo, alisema kwamba ujenzi wa Scanner katika geti kuu la kuingia uko mbioni kujengwa.
 
Akizungumzia mchakato wa zabuni, alisema kabla ya kutangazwa kwa kandarasi hiyo, zipo kampuni zilizojitokeza huku zikianisha gharama kubwa Na kueleza Kampuni ya StarFix iliyoshinda zabuni hiyo ilitumia shilingi bilioni 1.2 kukamilisha kazi husika.
 
‘’Kampuni ya kwanza iliandika andiko la shilingi bilioni 83, la bilioni 76, la tatu bilioni 33, la Nne bilioni 27 lakini huyu mzalendo Kampuni ya Starfix Enterprise ametumia gharama ya Shilingi Bilioni 1.2. Uwekezaji huu wa Serikali kwa pamoja umegharimu takriban kiasi cha shilingi bilioni 4.284,923,915.98,’’ alisema Prof. Msanjila.
 
Akielezea kazi nyingine zilizofanyika katika eneo hilo, Prof. Msanjila alisema Wizara imekamilisha ujenzi wa jengo la Kituo cha Pamoja ndani ya Ukuta, uwekaji miundombinu ya umeme na taa kuzungukia Ukuta umekamilika.
 
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Timu ya Wataalam waliosimamamia kufungwa kwa mradi huo akieleza namna kamera hizo zinavyofanya kazi alisema kuwa, zina uwezo wa kuhakikisha maeneo yote ya ukuta pamoja na maeneo mengine ikiwemo Geti Kuu la kuingilia, chumba cha kuthaminisha madini na vyumba vingine vinaonekana muda wote. Kituo Maalum (CCTV Control Room) cha uangalizi wa mienendo mbalimbali inayooneshwa na kamera zilizofungwa kimekamilika na kuanza kufanya kazi.
 
‘‘Mfumo uliyofungwa una uwezo wa kuonesha maoneo yote vilevile uwezo wa kufanya kazi Kwenye mazingira yote wakati wa mvua, jua Kali, vumbi, hivyo kutoruhusu Tukio lolote kupiga bila kurekodiwa, unauwezo kwa kutoa taaifa mubashara kwa wanaousimamia pindi kuna mtu anaporuka ukuta au matukio yaliyoanishwa kwenye mfumo kama hatarishi,’’ alisisitiza Moshiro.
 
Pia, alieleza kuwa, mfumo huo unao wezo wa kuwabaini wale wote waliokwishafanya matukio ya uhalifu pindi wanapotaka kuingia kwenye lango kuu au wanapotaka kutoka nje ya eneo.
 
Naye, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kuejnga Taifa Dkt. Faraji Mnyepe  akipokea Mfumo  huo alisema kuwa,yapo manufaa yanayotokana na kufungwa kwa kamera hizo  ikiwemo kukuza Pato la Taifa kutokana na udhibiti uliokuwa unafanywa wasio waaminifu.
 
Alissitiza kuwa,  wizara hiyo itaimarisha usalama kuzunguka Migodi yote, na kueleza kuwa jukumu la kulinda Usalama usalama ni la wizara hiyo na hivyo kuwahakikishia wachimbaji wote wadogo na Wakubwa usalama.
 
‘’Shahidi wa hili   ni bilionea Saniniu Lazier. Tulimlinda tangu kuzalisha hadi anauza  madini yake. Tunawaomba Wananchi na watanzania wote kulinda Madini Yetu, rasilimali ni jukumu letu wote. Ni malengo yangu wananchi wa Mirerani mtatusaidia kulinda Rasilimali hii,’’ alisema Dkt. Mnyepe.
 
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro Mhandisi Zephania Chaula alichukua fursa hiyo kuwaalika wawekezaji katika Wilaya hiyo na kuelezea kuwa, mbali tanzanite wizara hiyo imebarikiwa kuwa na madini mengine ikiwemo Green garnet.
 
Mbali na kukabidhiwa kwa mfumo huo, Afisa Mahusiano na Mawasiliano wa Kampuni ya StarFix  Jason Kyando iliyofunga kamera hizo, alisema kuwa,
 
 
baada ya zoezi la kufunga mfumo kukamilika tulitoa mafunzo kwa wasimamizi wa mfumo huo ambao wote ni vijana wa Kitanzania  walipatiwa mafunzo ya namna ya kusimamia mfumo huo na katika hafla ya jana Watapatiwa vyeti vya kuhitimu mafunzo hayo.