Rais wa Shirikisho la soka barani Afrika {Caf} Ahmad amepigwa marufuku ya miaka mitano na shirikisho la soka duniani Fifa kwa kukiuka sheria kadhaa za maadili.

Makamu huyo wa rais wa Fifa mwenye umri wa miaka 60 amedaiwa kukiuka sheria ya maadili inayohusisha jukumu lake la utiifu, kwa kutoa na kupokea zawadi hatua ambayo ni kinyume na wadhfa wake mbali na utumizi mbaya wa fedha.

Uchunguzi kuhusu tabia ya Ahmad kutoka mwaka 2017 hadi 2019 ulihusu masuala ya utawala wake katika shirikisho hilo pamoja na kuandaa na kufadhili safari ya kuhiji Mecca ya Umrah, kuhusishwa kwake katika kashfa ya kampuni ya vifaa vya michezo ya Tactical Steel na shughuli nyengine , ilisema taarifa ya Fifa.

Bwana Ahmad ambaye marufuku yake awali ilikuwa imetangazwa na BBCSport Africa , mwezi uliopita pia amepigwa faini ya $200,000.

Hapo awali alikana kufanya makosa yoyote.

Mwezi uliopita makamu huyo wa rais wa Fifa kutoka taifa la Madagascar alitangaza lengo lake kuwania muhula wa pili wakati uchaguzi wa Caf utakapofanyika mwezi Machi mwaka ujao.

Hilo huenda lisifanyike kwasababu atalazimika kupita mtihani wa maadili ili kustahiki kusalia katika baraza la Fifa.

Uwezekano wa yeye kuchaguliwa ka awamu ya pili utategemea iwapo atashinda kesi ya rufaa aliowasilisha katika mahakam ya kutatua mizozo ya michezo CAS , huku kesi hiyo akihakikisha kuwa inasikilizwa mapema ili kumruhusu kuthibitishwa kuwa mgombea.