Chama cha Wananchi (CUF), kimesema hakitashiriki tena katika Uchaguzi Mkuu mpaka itakapopatikana Tume Huru ya Uchaguzi

Pia, chama hicho kimesema hakikubaliani na matokeo yaliyotangazwa katika uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba 28, mwaka huu.

Kwa mujibu wa CUF, uamuzi huo umetokana na Kamati ya Uongozi ya Baraza Kuu la Uongozi la Taifa na Kamati ya Utendaji ya Taifa ya chama hicho iliyofanya kikao cha pamoja cha dharura kutathmini mwenendo na matokeo ya uchaguzi huo, Novemba 2, mwaka huu.

Akitoa tamko hilo jijini Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba, alisema kuanzia sasa kwa kushirikiana na wadau wengine, kitajikita katika kuwahamasisha Watanzania kupigania Katiba mpya.

Profesa Lipumba alisema chama hicho kimepanga kufanya maombi maalum siku ya Alhamisi wiki hii.

“Tunawaomba Watanzania wote wanaopenda haki nchini kote, kufanya ibada maalum siku ya Alhamisi, kwa kufunga kula mchana na kufanya dua na maombi baada ya kufungua, kila mtu kwa imani yake,” alisema Profesa Lipumba.