Rais wa zamani wa Marekani Barack Obama amesema, matokeo ya uchaguzi wa mwaka huu yamedhihirisha kuwa, kuna mpasuko mkubwa wa tofauti ndani ya nchi hiyo.

Akizungumza katika mahojiano na televisheni ya CBS, Obama ameashiria matokeo ya uchaguzi wa rais wa Novemba 3 na akaeleza kwamba, kupata kila mgombea kura zaidi ya milioni 70 kunaonyesha mpasuko mkubwa wa tofauti zilizoko ndani ya nchi.

Katika mahojiano hayo na CBS, Barack Obama amesema ni jambo la "kuvunja moyo" kwa kutochukuliwa hatua za kukabiliana na madai yasiyo na msingi ya kufanyika udanganyifu katika uchaguzi yaliyotolewa na rais Donald Trump ambaye pia ni mgombea urais kwa tiketi ya  chama cha Republican.

Tangu yalipotangazwa matokeo ya uchaguzi wa rais wa Marekani, akthari ya vyombo vya habari vya nchi hiyo ikiwemo hata televisheni ya Fox News inayomuunga mkono Trump vimemtangaza Joe Biden kuwa ndiye anayeongoza katika kinyang'anyiro cha urais.

Licha ya Biden, aliyegombea kwa tiketi ya chama cha Democratic kutangazwa mshindi wa uchaguzi wa rais wa Marekani, Trump hadi sasa hajayakubali matokeo ya uchaguzi na amesisitiza mara kadhaa kuwa, umefanyika udanganyifu mkubwa katika uchaguzi huo..

-Parstoday