Mahakama katika Jimbo la Pennsylvania imetupilia mbali kesi iliyofunguliwa na Donald Trump kupinga matokeo ya uchaguzi ambayo ilikuwa inataka kura zilizopigwa kwa njia ya posta katika jimbo hilo zifutiliwe mbali.

Jaji Matthew Brann alisema kesi haikuwa na “msingi wowote” wa kuthibitisha madai ya wizi wa kura.

Hatua hiyo inawezesha Rais mteule, Joe Biden anayeongoza kwa zaidi ya kura 80,000kuidhinishwa kuwa mshindi wa jimbo la Pennsylvania.

Hili ni pigo jipya kwa Trump ambaye anajaribu kupinga matokeo yanayoonesha kuwa alishindwa katika Uchaguzi Mkuu wa Novemba 3.

Trump amekataa kukubali kushindwa kwenye uchaguzi huo kwa madai kwamba kulikuwa na wizi wa kura bila ya kutoa ushahidi wowote.

Biden alimshinda Trump kwa kura 306 dhidi ya 232 za wajumbe ambazo ndio huamua nani anakuwa rais wa Marekani.