KIUNGO Mshambuliaji wa Yanga, Carlos Carlinhos anatarajia kuukosa mchezo wa dabi ya Simba na Yanga utakaochezwa Jumamosi ijayo huku kiungo Haruna Niyonzima, akirejea kwa nguvu kuwavaa watani wao hao.

Calinhos aliumia kisigino katika mazoezi yaliyofanyika hivi karibuni kwenye kambi ya timu hiyo AVIC Town iliyopo Kigamboni jijini Dar kulikosababisha akose michezo minne hadi sasa dhidi ya Polisi Tanzania, KMC, Biashara United na Gwambina.

Aidha Niyonzima ambaye alikuwa akisumbuliwa na Malaria, amesharejea tayari kwa kujiandaa na mechi ya watani Jumamosi.

Akizungumza na Championi Jumatano, Daktari wa Yanga, Shecky Mngazija amesema kuwa, hali ya kikosi hicho ipo vizuri majeruhi wote wamekaa sawa akiwemo Niyonzima ambao wapo naye Mwanza isipokuwa Carlinhos ambaye yeye alibaki Dar.

“Carlinhos hatoweza kucheza mechi ya watani wa jadi Simba na Yanga kwa kuwa hayupo na kikosi kwa muda mrefu hajafanya mazoezi, lakini kiafya anaendelea vizuri, hivyo hatakuwa sehemu ya kikosi kitakachoivaa Simba na kuwa hajafanya mazoezi.

“Niyonzima yeye amerejea kikosini ameshaanza mazoezi yupo fiti, hivyo suala la kupangwa ama kutopangwa katika mchezo huo ni jukumu la kocha,” alisema Mngazija