Mgombea ubunge wa jimbo la Kigoma mjini, kupitia chama cha ACT Wazalendo Zitto Kabwe, anatarajiwa kuendelea na kampeni zake kama kawaida kwa siku zijazo baada ya jana kuruhusiwa kutoka hospitali alikokuwa akitibiwa baada ya kupata ajali akiwa mkoani Kigoma.

Kupitia ukurasa wake wa Twitter , Zitto ameandika ujumbe wa kuwashukuru wauguzi wote walioshiriki kumpatia matibabu baada ya kupata ajali hiyo.

"Nimeruhusiwa kutoka hospitali, nawashukuru madaktari na wauguzi wa kituo cha afya Kalya, Uvinza, Hospitali ya Maweni Kigoma na Hospitali ya Aga Khan Dar es Salaam, ahsanteni sana wote kwa Dua, sala na maombi yenu, nataraji kurudi kwenye kampeni siku chache zijazo In Sha Allah", ameandika Zitto Kabwe.

Jumanne ya Oktoba 6 mwaka huu kiongozi huyo wa chama cha ACT Wazalendo na wenzake 4 walipata ajali ya gari maeneo ya Kigoma Kusini, ambapo kutokana na majeraha aliyoyapata alisafirishwa hadi jijini Dar es Salaam kwa ajili ya matibabu zaidi.