Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Innocent Bashungwa amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Prof. Riziki Shemdoe kufika kwenye kiwanda cha maziwa kinachojegwa kihanga, Karagwe ili kutatua changamoto anazozipata Mwekezaji wa kiwanda hicho.

Waziri Bashungwa ametoa maagizo hayo leo Oktoba 03,2020  alipotembelea na kukagua ujenzi wa kiwanda cha kuchakata maziwa cha Kahama Fresh kinachojengwa eneo maalum la viwanda lililopo Kihanga, wilaya ya Karagwe, Mkoa Kagera.

“Namuagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara kufika hapa Kihanga Karagwe kwenye kiwanda cha maziwa kinachojengwa, akiambatana na Idara ya Maendeleo ya Viwanda na taasisi za NARCO, TIC, EPZA, TARDB, TANESCO pamoja na taasisi nyingine Katibu Mkuu atakazoona Zinafaa kumsaidia mwekezaji ili kuhakikisha kiwanda hiki hakikwami” amesema Bashungwa

Waziri Bashungwa amepongeza jitihada za mwekezaji mzawa wa Kahama Fresh Limited, Bwana Jossam Mtangeki kwa kusaidia utekelezaji wa dira Serikali ya awamu ya tano katika ujenzi wa uchumi wa viwanda maana kwa mkoa hapakuwa na kiwanda cha maziwa chenye ukubwa wa kuchakata lita 10,000 kwa siku.

Sambamba na hayo, Waziri Bahungwa amefurahishwa na mpango wa uwekezaji ambapo kutakuwa na kiwanda kinachotengeneza vyakula vya ng’ombe wa maziwa pia amepongeza kwa kuwepo kwa shamba la ngo’ombe wa mfano ambalo linawasaidia wafugaji wadogo wadogo kupata elimu ya ufugaji wa ng’ome wa maziwa.

Aidha, Waziri Bashungwa amejadiliana na mwekezaji  mpango wa kugawa ngo’ombe kwa wafugaji wadogo wadogo na namna ya kuwasaidia wafugaji hao ili kupitia Serikali, Wizara ya Viwanda na Biashara na Wizara na wizara ya Kilimo ziweze kuwaweka hao wafugaji wadogo wadogo katika mfumo wa ushirika ili huduma za vyakula vitakavyozalizwa na kiwanda hicho viweze kuwafikia kupitia ushirika wao, ili serikali kupitia taasisi zake ziweze kuwasaidia wafungaji hao wa ng’ombe za maziwa ndani ya wilaya karagwe ili waweze kuuza maziwa yao kwenye kiwanda kinachoendelea kujengwa.

Nae Mkurugenzi wa kampuni ya Kahama Fresh Limited, Jossam Mtangeki ameishukuru Serikali Kupitia Waziri wa Viwanda na Biashara kwa kuendelea kuwewekea mazingira mazuri ya uwekezaji kwa kutenga maeneo maalum ya viwanda kwa kila wilaya na kuwasogezea mahitaji muhimu ambayo yanahitajika katika uwekezaji wao.

Jossam wakati akitoa taarifa ya kiwanda kwa Waziri Bashungwa amesema kuwa ujenzi wa kiwanda hicho umefikia kiwango cha kujenga majengo ya ofisi na kusawazisha eneo kitakapojegwa kiwanda na kiwanda kitakamilika ndani ya miezi sita na kitakuwa na uwezo wa kuchakata Lita 10,000 kwa mzunguko mmoja na gharama za ujezi mpaka kukamilika ni Billioni 2.4

Aidha, Jossam ametoa wito kwa wafugaji wa ng’ombe wa maziwa kuitumia fursa hiyo ya kiwanda hicho kukabiliana na changamoto ya soko la maziwa ambalo lilikuwa ni tatizo la muda mrefu, ambapo amewaomba wafugaji wa mkoa kagera kujikita na kuendelea kufuga ng’ombe wa maziwa kwa tija ambao utasaidia kiwanda hicho kufanya kazi pia na wao kunufaika kupitia uwepo wa soko la uhakika la maziwa kupitia kiwanda hicho.


MWISHO
Imetolewa na:
Kitengo cha Habari na Mawasiliano,
Wizara ya Viwanda na Biashara,
03 Oktoba, 2020