SERIKALI imeridhia kutoa hekari 1,625 kwa wananchi kutoka katika ardhi inayomilikiwa na Jeshi la Magereza Kijiji cha Ilagala Wilaya Uvinza mkoani Kigoma kwa lengo la kuendeleza kilimo cha zao la michikichi, pamoja na shughuli nyingine ikiwemo makazi.

Akisoma tamko la serikali kwa niaba ya Waziri Mkuu, Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Kamishna wa Polisi Thobias Andengeye, amesema hatua hiyo inalenga kumaliza mgogoro wa ardhi uliokuwepo baina ya wananchi wa kijiji hicho pamoja na Jeshi la Magereza tangu mwaka 1995.

Gereza la Ilagala lina ukubwa wa hekari 15,000 ambapo ni miaka mingi, baadhi ya wananchi wamekuwa wakivamia eneo hilo na kuanzisha makazi pamoja na shughuli za kilimo, hivyo kuhatarisha usalama wa eneo la gereza jambo ambalo serikali imeona ni bora kugawa sehemu ya eneo hilo.

Kamishna Andengenye amesema, wananchi watakaopata ardhi ambayo itakuwa ikipakana na Jeshi la Magereza, watakuwa walinzi wa mipaka ili wengine wasiweze kuvamia eneo lingine la magereza ambapo upatikanaji wa eneo hilo, itakuwa chachu ya wananchi kuendelea kufanya shughuli zao za uzalishaji wa uchumi.