Rais mstaafu wa Tanzania, Jakaya Kikwete amewataka wananchi kuchagua wagombea wa CCM katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 28, 2020 kwa kuwa chama hicho tawala kina sera nzuri na kinazitekeleza.


Kikwete ametoa kauli hiyo jana Jumamosi Oktoba 17, 2020 Mbagala jijini Dar es Salaam wakati akimuombea kura mgombea urais kupitia CCM, John Magufuli na kuwanadi wagombea ubunge wa chama hicho, Abdallah Chaurembo (Mbagala) na Doroth Kilave (Temeke).


Amesema sera nzuri za chama hicho zimeunganisha Taifa la Tanzania na kujenga umoja, undugu na upendo.


Amesema CCM ina sifa ya kuchaguliwa kutokana na kuwa na ilani nzuri ya uchaguzi yenye changamoto zote zinazowakabili wananchi.

“Rais Magufuli kapambana na rushwa, mahakama ya mafisadi imeanzishwa ndio manaa uchaguzi huu sijasikia mgombea yeyote aliyezungumza rushwa na atakeyechukua kama ajenda atakua ameishiwa,” amesema Kikwete.


Kikwete amewaomba wananachi wa Temeke na Mbagala wamchague tena Rais Magufuli ili amalize kazi aliyoianza katika awamu yake ya kwanza ya uongozi, ikiwemo ujenzi wa vituo vya afya na hospitali, barabara, usambazaji maji na umeme na huduma nyingine za kijamii.


“Tumchague Magufuli aendelee kuongoza nchi yetu, tumpe miaka mitano mingine amalize ngwe yake. CCM ina sera nzuri za kudumisha masilahi ya kisiasa, kijamii, kitamaduni, kiusalama na watu wake. Hakuna chama kingine kinachofanana na CCM mimi sikijui,” amesema Kikwete.