Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamis Kigwangalla, ameagiza Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA), kujipanga upya kwa kuwa na utayari wa kukabiliana na majanga ya moto yanapotokea katika maeneo ya hifadhi nchini.

Ametaka shirika hilo kwa kushirikiana na Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro (KINAPA), kununua helikopta yao maalum itakayokuwa ikitumika kukabiliana na majanga ya moto kisayansi zaidi.

Maelekezo mengine aliyoyatoa baada ya kupokea taarifa kuhusu tathmini ya udhibiti wa moto uliozuka katika Mlima Kilimanjaro Oktoba 11 mwaka huu, ni pamoja na kuwekeza katika uboreshaji wa miundombinu ya kuzimia moto mlimani.

Akiwa katika Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro jana, Dk. Kigwangalla alitembelea eneo lilioathiriwa na moto na kubainisha kuwa asilimia 1.6 ya hifadhi ya mlima huo ndiyo imeathirika na moto huo.

Alisema matukio ya moto yamekuwa yakitokea kwenye mlima huo, lakini uzimaji moto umekuwa ukifanyika kwa kutumia zana za kizamani, hivyo kusababisha moto kuchukua muda mrefu na kuleta madhara makubwa.

Waziri huyo alisema moto huo umeathiri eneo la ukanda wa tatu kati ya kanda tano za mlima huo.