Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imemhukumu Issa Mohhamed (27) miaka saba jela katika makosa 11 ikiwemo la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na kujitambulisha na kutumia jina la Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.

Hukumu hiyo imetolewa  Oktoba 2,2020 na Hakimu Mkazi Augustina Mmbando ambapo upande wa mashtaka umethibisha kwamba mshitakiwa alitenda makosa hayo.

Katika kesi hiyo washtakiwa wengine ni Nicholaus Joseph,Hamis Tembo na Wakati Mwichande ambao hawakukutwa na hatia yoyote.

Kwa mujibu wa hati ya mashtaka inadaiwa Kati ya Machi 10 na 17,2016 ndani ya Wilaya ya Ilala jijini Dar es salaam, mshtakiwa alijitambulisha kama Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, ambapo pia alighushi barua ikionesha imetoka ofisi ya Waziri Mkuu kwenda kwa makampuni tofauti ikiwataka kutoa Milioni 25 za Kitanzania kama punguzo la kodi.

Aidha mshtakiwa huyo baada ya kupata dhamana alitoroka hivyo anatafutwa kwa ajili ya kutumikia adhabu hiyo.