Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Simon Sirro, amewataka viongozi wa siasa, tume na wadau wengine wa siasa kutimiza wajibu wao katika kulinda amani ya nchi wakati huu wa uchaguzi.

“Tunatarajia kumpata rais mmoja atakayechaguliwa na wananchi hivyo kila mmoja ahakikishe anatimiza wajibu wake kudumisha amani iliyopo.”- Amesema IGP Simon Siro leo Oktoba 27 jijini Dar es Salaam alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu taarifa za vikundi vya watu wanaotaka kufanya vurugu.

Ameongeza kuwa jeshi la Polisi limejiandaa kuhakikisha amani ya nchi inaendelea kulindwa huku akiwasisitiza wapiga kura, kwenda kupiga kura bila woga nakuepuka vurugu katika vituo vya kupigia kura. 

Aidha,IGP  Sirro amesema kuna watu 42 waliokamatwa kisiwani Pemba wakidaiwa kuwashambulia polisi waliokuwa wakisambaza masanduku ya kura jana.

"Kama kule Zanzibar, wakati askari wanasambaza masanduku ya kupigia kura, kuna vijana walianza kurusha mawe na wameshulikiwa. Wapo karibu 42. Mpaka sasa hakuna kifo chochote," amesema IGP Sirro.