Na Avitus Benedicto Kyaruzi, Bukoba Kagera.
Wamiliki wa  viwanda vya kahawa Mkoani Kagera wametakiwa kutafuta soko  la ndani la zao hilo ili kuwajengea wananchi kutumia kahawa wanayozalisha wao.

Hayo yalisemwa na Katibu Tawala wa mkoa huo Profesa Faustine Kamuzora mnamo Agosti 5 mwaka huu wakati alipofanya ziara ya kutembelea kiwanda hicho cha AMIRAMZA kIlichopo katika halmashauri ya Wilaya ya Bukoba na kuongeza kuwa wamiliki wa viwanda vya kahawa wakitafuta soko la ndani itakuwa vizuri kwa kuwa itakuwa chanzo cha kuongeza watumiaji wa kahawa mkoani hapa kutokana na watu walio wengi kutokuwa na utamaduni huo.

Profesa Kamuzora amesema kuwa kwa kipindi hiki cha COVID 19 soko la kahawa lilitakiwa kuwa kubwa zaidi kwa upande wa soko la ndani kwa kuwa soko la Tanzania alijafungwa kama zilivyo nchi za nje na kuongeza kuwa kahawa inayozalishwa hapa nchini ni bora na ina vionjo ambavyo wakati mwingine haipatikani kokote duniani.
 
Amemtaka Mkurugenzi mtendaji wa kiwanda hicho bwana Amir Hamza kutumia utaalamu wake alionao kutengeneza soko la ndani ambalo litaongeza idadi kubwa ya watu kutumia zao hilo kwa upande wa mkoa huo.
 
“Watanzania walio wengi hasa wana Kagera hawana utamaduni wa kunywa kahawa mara kwa mara wakati sisi wenyewe ni wazalishaji wazuri wa kahawa na itakuwa vizuri ukianzisha migahawa ya kahawa ili wananchi wa mkoa huu wapate elimu ya kutosha juu ya matumizi ya kahawa”. Alisema Prof Kamuzola.
 
 Ili kuakikisha kwamba kahawa inayolimwa mkoani hapa inamunufaisha mkulima Prof Kamuzola amesema kuwa serikali imefungua milango kwa wanunuzi binafsi wa kahawa kwa kufuata vigezo na masharti yaliyowekwa ilimradi wasiharibu utaratibu uliopo.
 
Kwa upande wake Amir Hamza mmiliki wa kiwanda hicho amesema kuwa kiwanda hicho kwa sasa kinakumbwa na changamoto mbalimbali ikiwemo Uelewa mdogo wa mradi kwa  taasisi za kifedha hapa nchini uku akisema kwamba nchi za nje zinaitaji vitu kama dhamana ya serikalini,Tatizo la umeme wa uhakika, miundombinu ya barabara ya kuingilia kiwandani bado ni changamoto, Athari za COVID 19 kutokana na masoko ya nje kuwa yamefungwa, gharama kubwa za uzalishaji utafutaji masoko pamoja na usambazaji nk.
 
Pamoja na kuwepo kwa changamoto hizo bwana Hamza amesema kuwa kiwanda hicho kimeweza kushiriki katika  maonesho mbalimbali ya  kibiashara ndani na nje ya Tanzania ikiwa ni kutangaza vyema Mkoa wa Kagera na Tanzania kwa ujumla katika mataifa mbalimbali kama Italia, Ujerumani, Dubai, Uingereza, Misri, Marekani, Afrika kusini nk.
 
Aidha bwana Hamza ameiomba serikali kuwapatia mkopo wa muda mrefu ili waweze kutimiza kikamilifu mradi wa kiwanda hicho pamoja na upanuzi kuendana na kasi ya dunia.