Na Shamimu Nyaki –WHUSM, MOROGORO
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison   Mwakyembe amevitaka Vyombo vya Habari Nchini kuendelea kudumisha na kulinda amani katika kipindi chote cha kampeni mpaka Uchaguzi Mkuu  kwa kuandika na kutangazia  umma habari ambazo zina ukweli.
 
Waziri Mwakyembe ameyasema hayo Agosti 18, 2020 a alipokua akifanya mahojiano na vyombo vya habari vya redio na runinga vinavyomililikwa na taasisi ya “ISLAMIC FOUNDATION” ambavyo ni redio Imaan na TV Imaan pamoja kuzungumza na Wadau wa Sekta ya Habari wa Mkoa wa Morogoro ambapo amesema wanahabari wana nafasi ya kulinda au kubomoa amani ya nchi kupitia kalamu zao kama wasipozitumia vizuri, huku akitolea mfano nchi ambazo ziliingia katika machafuko kupitia vyombo vya habari.
 
“Mwanahabari ni mwalimu, mfasili, mkalimani, mchambuzi na mtetezi hivyo ni vizuri akatumia taaluma yake vizuri katika kuhabarisha umma ili asilete migogoro, Pia mwanahabari anapaswa kuelezea sera za wagombea na vyama vyao ili kuisaidia jamii kutambua mgombea sahihi na kuchagua mgombea bora”,alisema Mhe. Mwakyembe.
 
Dkt. Mwakyembe ameongeza kuwa kuwa ifikapo mwaka 2021 hakuna Mwandishi wa Habari yoyote ambaye kama atakuwa hajakidhi vigezo vya Sheria ya Huduma ya Habari ya mwaka 2016 pamoja na kanuni zake za mwaka 2017, ataruhusiwa kufanya kazi ya uandishi wa habari, lengo likiwa ni kuifanya taaluma hiyo kutambulika na kuheshimika.
 
Katika hatua nyingine Waziri huyo alipozumgumzia usikivu wa Shirika la Utangazi Tanzania TBC amesema kwamba Serikali imeimarisha usikivu wa shirika hilo ambapo mpaka sasa usikivu ni zaidi ya asilimia 70 na matarajio ni kufikia maeneo yote ndani ya mwaka huu wa fedha.
 
Kwa upande wake Mhandisi  Mkuu wa Shirika hilo Bibi.Upendo Mbelle amesema katika kuimarisha usikivu wa TBC mkoani Morogoro  Shirika linajenga kituo eneo la Kisaki  na kuweka mtambo wa Kilo Wati moja ( KW 1) ambacho kikimalilika mkoa wote wa utasikia,huku akeleza kuwa eno la Mlimba litawekwa mtambo ambao tayari umeshaagizwa na mkandarasi ameanza kufanya kazi.
 
“Morogoro ina changamoto ya milima na mambonde, lakini tukimaliza kuweka mitambo katika maeneo hayo usikivu hautakuwa na shida tena, na baada ya kazi hiyo tutafunga mtambo mdogo katika Wilaya ya Gairo”, alisema Bibi Upendo.
 
Vilevile Mkuu wa Mkoa wa Mororgoro Mhe.Loata Olesanare amesema mkoa huo unafanya vizuri katika sekta zote za Wizara hiyo ikiwemo kuhifadhi na kulinda mila na desturi pamoja na kulinda maeneo yote ya kiutamaduni yalipo mkoani hapo.
 
…MWISHO..