Ni miongo miwili sasa tangia Vodacom ianze kutoa huduma za mawasiliano nchini Tanzania. Muriel Rukeyser (1913 - 1980), mshairi wa kimarekani, alipata kusema; “ulimwengu unaumbwa kwa simulizi, na sio atomu”. Makala hii ni simulizi kuhusu kampuni hii kubwa ya mawasiliano nchini Tanzania.

Kama umekuwa mdadisi wa sekta ya mawasiliano nchini Tanzania kwa miongo miwili ama zaidi, unaweza kukubaliana nami kuwa kumekuwepo na mijadala na maswali kadhaa juu ya ulipaji kodi wa makampuni ya simu hapa Tanzania. Mara nyingine kumekuwa na utata. Ni kwa kiasi gani kampuni za mawasiliano,Vodacom ikiwemo, zinalipa kodi nchini Tanzania? Pengine hilo ni mojawapo ya maswali muhimu. Fuatana nami katika makala haya.

Vodacom ndio kampuni kubwa zaidi miongoni mwa makampuni ya mawasiliano zaidi ya nusu dazeni hapa Tanzania. Ripoti ya karibuni ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), inaonesha kuwa mpaka mwezi Machi 2020, makampuni ya simu yanahudumia wateja (unique subscribers) zaidi ya milioni 48. Katika hao, Vodacom inaongoza kwa kuwa na wateja milioni 15 (asilimia 32 ya soko). M-PESA ya Vodacom pia ni chapa inayoongoza. Inahodhi asimilia 39 ya soko.
Chanzo: Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania, Machi 2020
Lakini, si watu wengi wanajua kuwa, kando ya ukubwa, Vodacom inajivunia pia kuwa miongoni mwa walipakodi vinara. Unajiuliza: sasa inakuwaje mtu anaweza kujigamba kwa kuwa mlipakodi mkubwa? Ukiwa mzalendo, inawezekana. Joyce Marcel, mwanahabari na mwandishi maarufu wa kimarekani, anasema, “kwa wazalendo, kulipa kodi kunafanya ujisikie kuwajibika, kuwa sehemu ya jamii, na kuchangia katika malengo ya pamoja ya wananchi”. Vodacom ni mojawapo ya wazalendo hao.

Kodi ni suala nyeti sana. Kwa wastani, kodi inayokusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ni karibia asilimia 60 ya bajeti ya serikali. Mwaka 2015 shirika la kimataifa la makampuni ya simu za mkononi, GSMA, lilitoa ripoti maalumu iliyohusu utozaji kodi katika sekta ya mawasiliano Tanzania (“Digital inclusion and mobile sector taxation in Tanzania”). 

GSMA ilikadiria kuwa makampuni ya simu za mkononi yanachangia zaidi ya asilimia 11 ya makusanyo ya kodi nchini Tanzania. Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, Vodacom imelipa serikalini kodi, ada na tozo mbalimbali zinazofikia shilingi trilioni moja na bilioni mia tisa. Ulipaji wa kodi wa Vodacom unakua kwa wastani wa asilimia 8 kila mwaka. Kutoka shilingi bilioni 324 mwaka 2016 mpaka kufikia shilingi bilioni 435 mwaka 2020.

Chanzo: Vodacom Tanzania Plc
Lakini, je, Vodacom imelipa kodi gani? Hili ni swali muhimu. Vodacom, kama kampuni, inawajibika kisheria kulipa kodi mbalimbali serikalini. Katika mafungu sita, nitataja baadhi ya kodi kubwa ambazo Vodacom imelipa kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita (2016 - 2020):

Kwanza ni kodi ya mapato ya makampuni. Vodacom imelipa jumla ya shilingi billion 221 katika miaka mitano iliyopita. Kwa mwaka 2016 ililipa shilingi bilioni 36. Lakini mwaka 2020 imeongezeka na kufikia shilingi bilioni 48.6. Sifikiri kama kuna kampuni zaidi ya nne hapa Tanzania zinazofikia au kuzidi kiwango hiki cha kodi kwa mwaka.

Vodacom pia imelipa jumla ya shilingi bilioni 525 kama kodi ya ongezeko la thamani; na shilingi bilioni 614 kama ushuru wa bidhaa katika miaka hiyo mitano. Mbali na kodi hizi, kuna kodi mbalimbali zinazohusiana na mishahara kwa wafanyakazi. 

Hii inajumuisha kodi ya mapato ya ajira, ushuru wa ujuzi, michango kwa mfuko wa fidia ya wafanyakazi, pamoja na michango kwenye mfuko wa taifa wa pensheni. Kwa ujumla wake, kwa miaka mitano, Vodacom imelipa shilingi bilioni 96.8 ya kodi zote hizi zinazohusiana na ajira.

Kodi ya zuio ni eneo jingine. Vodacom imelipa TRA jumla ya shilingi bilioni 163.6 kama kodi ya zuio katika kipindi cha miaka mitano. Zipo pia ada na kodi mbalimbali zinazolipwa kwa Benki Kuu (BOT), TCRA, na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF). Vodacom imelipa kwa taasisi hizi za udhibiti jumla ya shilingi bilioni 178 katika miaka mitano iliyopita.

Bila kutaja viwango, itoshe kusema kuwa hiyo shilingi trilioni mbili kasoro inajumuisha pia kodi, ada na tozo kadhaa zilizolipwa kwa halmashauri au taasisi za serikali. Ushuru wa huduma (service levy), ushuru wa forodha (import duty), kodi za majengo, kodi za ardhi, kodi za mabango na ada za leseni za biashara, kwa kutaja baadhi. Mbali na faida hizi za kikodi, kuna faida zingine zinazoletwa na makampuni ya simu? Tuendelee.

Simu za mkononi ni sehemu ya maisha yetu kwa sasa. Haziepukiki. Pengine, janga la corona (COVID-19), limeonesha vizuri zaidi umuhimu wa sekta ya mawasiliano, hususani simu za mkononi. Watu kutotangamana (‘social distancing’), kama mojawapo ya njia kuu za kuzuia kusambaa kwa maambukizi ya COVID-19, ni rahisi zaidi kutekelezwa pale watu wanapoweza kubakia nyumbani lakini bado wakaweza kuwasiliana kwa simu za mkononi. GSMA, katika ripoti yake inataja faida mbalimbali zitokanazo na kukua kwa huduma za simu za mkononi hapa Tanzania.

Moja ni ujumuishwaji wa wananchi kidigitali. Ukweli kwamba watanzania, kwa mamilioni, sasa wanaweza kuzifikia na pia kunufaika na huduma za simu za mkononi. Ujumuishwaji wa wananchi kwenye mifumo ya kifedha ni faida ya pili. Yaani, watu wengi zaidi wanaweza kupata huduma za kifedha na za kibenki kupitia simu zao. 

Kwa mfano, kwa kutumia M-Pesa, watu wengi zaidi na kwa urahisi wanaweza kulipia bili mbalimbali, kufanya miamala ya biashara na kubwa zaidi kulipa kodi za serikali. Faida ya tatu GSMA inaitaja, ni ukuaji na utulivu wa kiuchumi. Huduma za simu zimewezesha bishara za ndani na za kimatatifa na hivyo kutoa mchango wa moja kwa moja katika uzalishaji na kukuza uchumi wa Tanzania.

 GSMA inataja eneo la nne kuwa ni huduma za simu kuwezesha serikali kufikia kwa ufanisi zaidi malengo yake ya TEHAMA na ya kijamii. Mwezi Desemba mwaka 2019, TRA iliweka rekodi ya juu kabisa ya ukusanyaji mapato. Ilikusanya shilingi trilioni 1.987. 

Matumizi ya mashine za EFD ni mojawapo ya sababu za mafanikio hayo. Mashine na mfumo wa EFD unategemea huduma za simu, hasa data. Pamoja na vifaa vingine, mashine ya EFD ndani yake inawekwa “laini ya simu” ili iweze kuwasiliana na mfumo uliopo TRA.

Vodacom ni kampuni pekee ya simu za mkononi mpaka sasa kutimiza takwa la Sheria ya Posta na Mawasiliano ya Kielektroniki, SURA 306 la kujisajili na kuuza asilimia 25 ya hisa zake kwa Watanzania katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE). Kuorodheshwa kwa Vodacom mwaka 2017, kuliwezesha watanzania zaidi ya 40,000, kununua hisa za Vodacom na hivyo kuwa sehemu ya wamiliki. Kuorodheshwa katika soko hilo pia kumeleta uwazi zaidi katika biashara ya Vodacom na masuala mengine hasa ya kodi.

Kipindi cha miaka ishirini ya Vodacom nchini Tanzania, kimepambwa pia na tuzo kadhaa. Hiyo ni katika kutambua mchango mkubwa wa Vodacom kiuchumi, kijamii na zaidi katika kodi. Kwa mfano, katika kilele cha siku ya walipakodi (7th Taxpayers’ Day) mwaka 2013, TRA iliitunukia Vodacom tuzo kubwa mbili. Kupitia tuzo hizo, TRA ilitambua mchango mkubwa wa kodi na utiifu wa Vodacom kwa sheria za kodi. Vodacom ilishika nafasi ya kwanza kisekta na nafasi ya tatu kitaifa.

Kuanzia katikati ya miaka ya 1990 mpaka sasa, sekta ya mawsiliano ya simu za mkononi nchini Tanzania imekua kwa kiasi kikubwa. Katika muongo mmoja uliopita pekee, idadi ya watumiaji wa huduma za simu imeongezeka maradufu na kufikia 48 milioni.

 Na katika kipindi hicho, Vodacom imekuwa mbele kabisa katika maendeleo hayo. Wigo wa huduma za simu za mkononi umepanuka sana, na ubora pia umeongezeka. Tulianza na huduma za kupiga simu na kutuma ujumbe mfupi wa maandishi pekee. 

Lakini, ubunifu na maendeleo ya teknolojia, yameleta huduma mpya za data na huduma za kifedha. Hizi zimebadili pakubwa taswira nzima ya sekta hii na umuhimu wake kwa watu na uchumi wa Tanzania. 

Bahati nzuri pia, ukuaji wa huduma ulienda sambamba na kushuka kwa gharama za huduma na hata simu za mkononi (handsets). Hii iliwezesha watanzania wengi zaidi, hasa wale wa vijijini, kumudu na kutumia huduma za simu za mkononi.
 
Kwa hivyo, Vodacom imekuwa mojawapo ya makampuni ya kizalendo kabisa. Bila shaka, Vodacom ni mwekezaji mkubwa, mwajiri mkubwa, mlipa kodi mkubwa na pia mnunuzi mkubwa wa bidhaa na huduma mbalimbali hapa nchini. Hii inachangia pakubwa katika kutengeneza thamani ya huduma na bidhaa nchini Tanzania.

Lakini, nini siri ya mafanikio haya? Mafanikio yote haya hayakuja kirahisi tu. Hasa kwa kuzingatia ukubwa wa kijiografia wa Tanzania. Ilihitaji uwekezaji mkubwa wa miundombinu. Lakini zaidi sera bora za uwekezaji na za kikodi. 

Ni kazi ya pamoja kati ya serikali na sekta binafsi na iliyohitaji kujitolea pakubwa. Kwa mfano, serikali haikupata kodi ya mapato kwa muda fulani kwa vile ilitoa motisha kubwa za uwekezaji. Serikali haikupata pia ushuru wa forodha. Lakini makampuni ya simu, Vodacom ikiongoza, yaliwekeza pakubwa. Kati ya mwaka 2012 na 2020, Vodacom pekee imewekeza zaidi ya shilingi trilioni 1.6 nchini Tanzania.

Kwa miaka ishirini nchini Tanzania, inafanya kwa vitendo yale inayohubiri. Vodacom inashirikiana kikamilifu na serikali - mfano, imetii takwa la kisheria la kujiorodhesha DSE. Sasa serikali kupitia mashirika ya hifadhi ya jamii inamiliki hisa za kutosha za Vodacom.

 Vodacom pia inaleta manufaa kwa watanzania - kwa kuleta ubunifu unaoleta tija kwa biashara, makampuni na watu binafsi; na zaidi kwa wafanyakazi wake zaidi ya mia tano na hamsini; bila kusahau ajira kwa mawakala zaidi ya laki moja kote nchini.