Baada ya kusambaa kwa picha zikimuonesha mwanamama wa Bongo Fleva, Esterlina Sanga ‘Linah’ akijiachia na mchezaji matata wa Simba, Benard Morrison, video vixen asiyeishiwa habari Bongo, Zena Abdalah ‘Jike Shupa’ ameapa kumg’oa jamaa huyo ili awe wake wa kudumu maishani.



Akizungumza na Gazeti la IJUMAA baada ya kunaswa kwa video yake akiwa kwenye bwawa la kuogelea na mwamba huyo, Jike Shupa ameapa kumkamata vilivyo jamaa huyo.

Jike Shupa amesema kuwa, ndiyo kwanza ameanza makeke yake na anaamini kabisa, Morrison ni mali yake.



Mrembo huyo aliyejipatia umaarufu baada ya kuuza nyago kwenye video ya Wimbo wa Jike Shupa wa msanii wa Bongo Fleva, Naftal Mlawa ‘Nuh Mziwanda’ amesema ‘tajeti’ yake ni kumuweka jamaa huyo kwenye himaya yake na anaamini muda si mrefu jambo hilo litatimia. Jike Shupa anasema kuwa, kinachompa matumani kwa staa huyo wa mpira ni kwamba, tayari jamaa ameanza kumpenda mtoto wake (Jike Shupa) aitwaye Kizy.



“Kama picha mmeliona ndiyo kwanza ni ‘trela’ bado picha yenyewe ya kibabe inakuja.
“Ninawapa mwezi mmoja tu, Morrison atakuwa mali yangu kwa sababu tayari ameanza kuonesha upendo kwa mwanangu Kizy; yaani yajayo yanafurahisha sana,” ametamba Jike Shupa akiahidi kumpa Morrison mavituz hadimu.
 

Kwa upande wake Linah, alipoulizwa na gazeti hili kama kuna chochote kinaendelea kati yake na Morrison alisema; “Mimi na Morrison ni washkaji tu, ninaweza kusema yeye ni shabiki yangu na mimi ni shabiki yake.

“Tulikutana katika mazingira f’lani ambayo hata mimi sikutegemea kama ningekuwa hapo.
“Morrison aliponiona alisema ni mwanamuziki anayenifuatilia kazi zangu tangu kitambo.
“Aliponiita nikaingia hiyo sehemu aliyokuwepo, alikuwa anacheza gemu na washkaji zake, tukapiga picha, siyo mpenzi wangu.”



Morrison ambaye hivi karibuni aligonga sana vichwa vya habari hapa nchini, kwa sasa ni mchezaji rasmi wa Simba SC baada ya kushinda shauri lake dhidi ya Yanga SC aliyokuwa akiichezea awali.