Habari kutoka kijiji cha Nyanguge Wilayani Magu Mkoani Mwanza zimethibitisha kufariki kwa Dkt Louis Shika ambaye alijipatia umaarufu mitandaoni baada ya kutangaza kutaka kununua nyumba za mnada huko Kigamboni kwa Shilingi Milioni 900.

Ndugu wa karibu wa marehemu  amesema ni kweli Dkt Shika alilazwa Katika Kituo cha Afya Nyanguge wilaya ya Magu mkoani Mwanza kwa siku kadhaa akipatiwa matibabu baada ya kuugua kwa muda mrefu lakini baadaye alitolewa hospitali na kurudishwa nyumbani ambapo  umauti umemfika jana .

Aidha wamesema taratibu za mazishi zinaendelea na kuna uwezekano mkubwa akazikwa leo Agosti 25, 2020 kijijini hapo.

Ikumbukwe tu kipindi cha nyuma zilitoka taarifa kwamba Dkt Louis Shika anahitaji msaada wa kifedha kwa ajili ya kufanyiwa matibabu kwa sababu alikuwa anasumbuliwa na matatizo ya kiafya.