Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Arusha
Waziri wa Kilimo Japhet Hasunga ametoa siku 14 kwa Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Nafaka na Mazao mchanganyiko Dkt Anslem Moshi kukamilisha malipo ya wakulima wote waliouza korosho msimu wa mwaka 2018/2019.

Waziri Hasunga ametoa agizo hilo wakati alipotembelea na kukagua shughuli za utendaji kazi zinazofanywa na Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko Jijini Arusha.

Amesema kuwa Bodi hiyo ilipewa dhamana la kununua korosho mwaka 2018 kwa niaba ya serikali na tayari serikali imeshatoa fedha zote kwa ajili ya wakulima lakini bado CPB haijakamilisha malipo hivyo ni lazima malipo yakamilike ndani ya siku hizo.

“Ndani ya siku 14 sitaki kusikia malalamiko ya wakulima lazima wakulima wote wawe wamelipwa fedha zao haraka iwezekanavyo” Alisisitiza

Katika ziara hiyo pia Waziri Hasunga amemuagiza Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Nafaka na mazao mchanganyiko kuwasilisha haraka mpango kazi wa namna viwanda hivyo vitakavyofanya kazi kwa ajili ya kutengeneza bidhaa zitakazohitajika na wateja na kukidhi matarajio ya serikali ikiwa ni pamoja na kuainisha idadi ya watumishi wanaohitajika.

Hasunga ameiagiza kampuni ya Monaban ambayo ilikuwa imekodisha kiwanda hicho kutekeleza maagizo ya serikali yaliyotolewa mwaka jana ya kuhamisha mali zao zote zilizopo katika eneo hilo la serikali kwani kesi mahakamani na notisi ilishaisha.

Akiwa kiwandani hapo Waziri Hasunga amebaini uchakavu wa mitambo iliyopo pamoja na uchache wa watumishi wanaofanya kazi katika kiwanda hicho hivyo ameagiza kufanyika ukarabati wa majengo hayo kuanzia mwezi Agosti badala ya Octoba kwa taasisi hiyo ilivyopanga.

“Tukisubiri mpaka mwezi wa kumi tutakuwa tumechelewa kwa kuwa mvua zitaanza kunyesha jambo ambalo litapelekea kushindikana kufanyika ukarabati” Amesema

Amesema kuwa Lengo la serikali ni kufufua viwanda kwa ajili ya kuongeza thamani ya mazao ya nafaka nchini ili kuzalisha bidhaa mbalimbali kama unga N,k na kuuza katika masoko ya ushindani ndani na nje ya nchi.

MWISHO