Chama cha wananchi CUF kimesema kuwa endapo kitashinda katika Uchaguzi Mkuu kwa ngazi ya Urais, kitaunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa ili kuimarisha demokrasia ya kweli na kuleta ushindani wa kisiasa nchini utakaotumikia Watanzania wote kwa misingi ya haki sawa.


 
Akifungua mkutano mkuu wa chama cha wananchi CUF, Mwenyekiti wa chama hicho Profesa Ibrahim Lipumba amesema, kwenye uchaguzi wa mwaka 1995, sera za chama hicho zilikuwa elimu bure, afya pamoja na kukuza uchumi wa nchi lakini badala yake CCM waliiba sera zake na baadaye aliitwa Profesa uchwara.

“Sera za CUF ni kuwafanya Watanzania kuwa na furaha furaha tunayoitaka  CUF ni ile ya wafanyakazi kupandishwa mishahara makazini, furaha ya kupata huduma bora za afya na maji katika eneo lao, furaha ya kumudu gharama za maisha kuendana na hali ya sasa, mwaka 1995 CCM waliniita Profesa uchwara na waliiba sera zetu ambazo wamezitekeleza kwa kiwango hafifu”, amesema Prof Lipumba.

Prof. Lipumba ameongeza, “Tumekusanyika hapa kufanya maamuzi yatakayotoa mustakabali mwema kwetu na waananchi kwa ujumla, ni mkutano mkuu wetu CUF , tutaamua kwa haki kama wajumbe, wajumbe waaminifu na watiifu, sisi sio kama wale wajumbe wengine”.