KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Bashiru Ally, amesema maandalizi ya mkutano mkuu wa CCM yamekamilika na kuwa mgombea wa Zanzibar atakayepatikana, wana uhakika atamshinda mgombea wa upinzani visiwani humo.
Alisema mchakato unaoendelea wa kumteua mgombea urais wa Zanzibar jijini Dodoma, ni suala linalofanyika kwa mujibu wa katiba ya chama hicho.
Dk. Bashiru alitoa kauli hiyo jana wakati akihojiwa na kituo cha Televisheni cha Uhai Tv.
Akijibu hoja ya mgombea urais wa Zanzibar kuchaguliwa na wajumbe wa Bara, Dk. Bashiru alisema huchaguliwa na wanachama wa CCM visiwani humo, kisha huthibitishwa na vikao vya chama, bila kujali wajumbe wake wanatoka Bara ama Zanzibar.
“Mchakato wa kupata mgombea urais wa Zanzibar huanzia uchukuaji fomu na wanaohusika ni wanachama wa CCM Zanzibar, baada ya hapo hatua ya uteuzi huanza, kuanzia vikao vya Halmashauri Kuu.
“Mchakato upo kwa mujibu wa katiba na unakidhi matakwa ya kikatiba ya CCM na ya nchi,” alisema Dk. Bashiru.
Alisema wenye mamlaka ya kumchagua Rais wa Zaznibar ni Wazanzibar wenyewe, ambao huchagua mtu wanayemtaka.
“Vyama vya siasa vinateua wagombea, vyama havichagui rais, Rais wa Tanzania huchaguliwa na Watanzania na wa Zanzibar huchaguliwa na Wazanzibar, kinachofanyika CCM ni mchakato wa uteuzi, si uchaguzi,” alisema Dk. Bashiru.
Alisema hana sababu za kujadili zaidi mjadala huo kwakuwa hautokani na wanachama wa CCM, bali unavumishwa na watu ambao si wanachama wa chama hicho.
“Hao sio wanaCCM, CCM wanaamini katika utaifa na umoja, ndani ya CCM kuna wanachama na si Zanzibar au Bara, kila mwanachma ana haki na wajibu sawa na kila wanapokaa ni kikao baina ya wanaCCM.
“Na kama si wanaCCM wanaotoa malalamiko hayo, sina sababu ya kujadili mawazo yao na hayawezi kuwepo.
“Siyo tu katiba hairushusu ubaguzi, lakini pia ndani ya CCM tunakuwa kama wanachama, na mambo yetu yanaendeshwa kama wanaCCM wanaoamini katika utaifa,” alisema Dk. Bashiru.
ORODHA NDEFU URAIS ZANZIBAR
Akizungumzia idadi kubwa ya makada waliochukua fomu ya kuwania urais wa Zanzibar, alisema hoja yake ilikuwa ni kwa namna gani makada hao wanafuata na kuzingatia kanuni za chama.
“Wakati nazungumza sikuwa nahangaika na idadi, nilikuwa nahangaika na utii wa kanuni na taratibu za chama, hata wangekuwa wawili, wakati huo walikuwa 12 na sasa wamerejesha 31 kati ya 32 waliochukua fomu.
“Wakati ule nilikuwa nawakumbusha wale wanaotaka kuwania nafasi hiyo kwamba uko utaratibu, na ziko kanuni, na kila mmoja analazimika kuzitii.
“Unajua tatizo siyo wingi wa wagombea, tatizo ni hisia za wagombea, uwezo wao na mienendo yao ambayo inaweza ikaimarisha au ikahatarisha umoja wa chama.
“Kwa hiyo msisitizo wangu ulikuwa bila kujali idadi ya watakaojitokeza, yeyote ambaye alitaka kugombea alitakiwa kufuata taratibu na kanuni za chama, kinyume na hivyo ilikuwa ni kudhohofisha demokrasia ndani ya chama na chama kingeweza kupoteza uwezo wa kushinda uchaguzi.
“Pia nakukumbusha kwamba ni kawaida kila rais wa CCM anapomaliza muda wake – awe wa Zanzibar au bara, wengi hujitokeza, kama ulifuatilia baada ya mzee Mwinyi (Ali Hassan Mwinyi Rais wa Awamu ya pili) alipohitimisha uongozi wake, walijitokeza wagombea wengi, hivyo hivyo kwa mzee Mkapa (Benjamini Mkapa, Rais wa awamu ya tatu) na Kikwete (Jakaya Kikwete, Rais wa awamu ya nne), sasa kwa upande wa Zanzibar mwaka huu, Dk. Shein anamaliza muda wake kwa mafanikio makubwa, ametii sheria za nchi na katiba ya chama anang’atuka, amemaliza muda wake, hivyo haishangazi kujitokeza kwa idadi hiyo ya wagombea 31.
“Kitu tunachokisisitiza kwa watu wanaojitokeza, watetee sifa zao na uwezo wao wa uongozi, lakini pia waweze kutii sheria na katiba ya nchi na chama ili chama chetu kiendelee kuwa na umoja na mshikamano, hayo ndiyo yalikuwa mawazo yangu ya wakati ule na wakati huu nikiwa mimi ndiye mtendaji mkuu wa kusimamia utaratibu na shughuli za chama,” alisema Dk. Bashiru.
Alisema kwa sasa hakuna lolote analolijua kuhusu mchakato wa kuwapata makada watano uliofanyika Zanzibar na kwamba atafahamu pindi vikao vitakapoketi.
Dk. Bashiru alisena maandalizi ya mkutano mkuu yamekamamilika na ajenda ni kupiga kura kumteua mgombea urais wa CCM.
Alisema kutakuwa na hotuba ya rais kuelezea majukumu yake na utekelezaji wa ilani, pia kutakuwa na taarifa ya Serikali zote mbili zinazoongozwa na CCM.
Kuhusu Rais Magufuli kutokuwa na mpinzani, alisema katika maisha ya binadamu kuna mambo ambayo yanatokea kisheria au mazoea na kuna mambo ambayo yanafanyika bila maandishi na yanakuwa mazuri zaidi.
“Hivyo siyo kila jambo linalofanyika linafanyika kutokana na sera za chombo husika, yako ambayo hayajaandikwa, yanafanya vizuri na yapo ambayo yameandikwa hayafanyi vizuri.
“Tangu utaratibu huu wa mihula miwili umeanza kwa mzee Mwinyi, tunaona unaenda vizuri hadi sasa na sitashangaa hata akija mrithi wa Dk. Magufuli 2025 akafanya vizuri basi ataendelea.
“Bahati nzuri nimekaa miaka miwili kwenye nafasi hii, ni muda wa kutosha, hivyo kungekuwa na shida kwenye hilo basi ningekuwa nimeshapata taarifa,” alisema Dk. Bashiru.
KUHUSU MEMBE
Alipoulizwa kuhusu aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje, Bernard Membe, ambaye amekuwa akidai alifukuzwa uanachama wa CCM kwa sababu ya kutaka kugombea urais kwa tiketi ya chama hicho, Dk. Bashiru alisema; “kwanza mazungumzo yetu yanahusu vikao vya uteuzi, ndilo jukumu lililoko mbele yangu, ambalo ni kubwa na zito, na kwa mara ya kwanza ndiyo nasimamia jukumu hili zito.