Licha ya kupata hati safi kwa kipindi cha miaka mitatu mfululizo Watendaji na Watumishi wa halmashauri ya Wilaya Missenyi Mkoani Kagera wametakiwa kuongeza udhibiti wa mapato yanayokusanywa ili kufikia malengo ya halmashauri hiyo.
Hayo yamebainishwa na Mkuu wa Wilaya Missenyi Kanali Denis Mwila kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera Brigedia Jeneral Marco Elisha Gauti alipo kuwa mgeni rasmi katika baraza maalumu la Madiwani wa halmashauri hiyo kwa kujadili hoja za mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa hesabu za Serikali CAG lililofanyika tarehe 03/062020.
DC Mwila ameitaka Halmashauri hiyo kuendelea kushirikiana katika changamoto zinazojitokeza ikiwa ni pamoja na kuongeza udhibiti wa mapato yanayokusanywa, kuimarisha usimamimzi na mfumo wa vyanzo vya mapato ya ndani, kuimarisha usimamizi wa rasilimali watumishi na fedha ili kuboresha malengo ya utoaji huduma kwa wananchi kwa kuzingatia maelekezo ya serikali na mpango wa bajeti ya halmashauri.
Kanali Mwila amesema kuwa kwa miaka mitatu Wilaya ya Missenyi imefanikiwa kusimamia vyema rasilimali za halmashauri katika wilaya hiyo jambo ambalo limepelekea Wilaya hiyo kupata hati safi kwa kipindi hicho uku akiwataka watumishi katika halmashauri hiyo kutobweteka na mafanikio hayo bali waendelee kuchapa kazi na kuongeza mapato ya halmashauri na taifa kwa ujumla.
Akitoa salamu za shukrani Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Mh Henry Bitegeko ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Gera (CCM) amemuomba mgeni rasmi kuendelea kuishauri halmashauri hiyo pale ambapo anaona kuna mapungufu na amemuhakikishia mgeni rasmi kuwa ushauri pamoja na maagizo yaliyotolewa yatafanyiwa kazi haraka iwezekanavyo ili kuweza kufikia malengo.
Ameongeza kuwa kuna baadhi mambo ambayo yashaanza kutekelezwa ikiwa ni pamoja na ukusanyaji wa mapato ya ndani uku akitaja mwaka 2018/2019 wilaya hiyo ilikuwa na79.5% na mwaka 2019/2020 halmashauri iyo katika ukusanyaji wa mapato ilikuwa 100%kufikia mwezi wa tano.
Mh Bitegeko amesema mafanikio waliyoyapata ni mshikamano kati ya watendaji pamoja na Madiwani wa halmashauri hiyo uku akimpongeza pia Rais Wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dk John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuendelea kuinua uchumi wa nchi.