Ijapokuwa tume ya uchaguzi ya Malawi MEC bado haujatangazwa matokeo ya uchaguzi wa urais uliorudiwa , ishara za mapema zinaonesha kwamba rais Peter Mutharika yuko nyuma ya mpinzani wake mkuu Lazarus Chakwera.

Kulingana na mgombea mwenza Atupele Muluzi, ambaye alisema kwamba ametumwa na Mutharika kuzungumza na vyombo vya habari, rais amewataka wafuasi wake kupuuza ripoti zinazosema ameshindwa katika uchaguzi huo, akisema wanapaswa kusubiri matokeo rasmi ya tume ya uchaguzi ya MEC.

Atupele Muluzi ni mwana wa rais wa zamani Bakili Muluzi na kiongozi wa chama kidogo cha upinzani United Democratic Party DPP.

Muluzi amedai kwamba takribani wachunguzi 15 waliotumiwa na DPP/UDP katika maeneo ya upinzani wametoweka na wengine kuhofiwa kufariki baada ya kushambuliwa na wafuasi wa upinzani.

Matokeo ya wilaya zote 28, yaliotiwa saini na maafisa pamoja na wawakilishi wa wilaya yanaonesha kwamba rais Mutharika yuko nyuma ya Lazarus Chakwera ambaye anaongoza chama cha upinzani cha Malawi Congress na kinawakilisha muungano wa Tonse unaoshirikisha vyama vinane vya upinzani.

Je ushindi wa upinzani Malawi una maana gani kwa demokrasia Afrika?
Chombo cha habari cha serikali kinasema upinzani unaongoza
Upinzani nchini Malawi unaelekea kupata ushindi katika kura ya uchaguzi wa urais inayofanyiwa marudio baada ya matokeo yake kufutiliwa mbali kufuatia madai mengi ya udanganyifu.

Matokeo rasmi ya uchaguzi huo uliofanyika siku ya Jumanne hayajatangazwa na tume ya uchaguzi ya Malawi.

lakini chombo cha habari cha serikali MBC kinasema kwamba kiongozi wa upinzani Lazarus Chakwera alikuwa anaongoza na asilimia 59 ya kura zilizohesabiwa siku ya Jumatano.

Rais Peter Mutharika , ambaye anawania muhula wa pili ana asilimia 38 ya kura zilizohesabiwa, kinasema.

Mgombea wa tatu ambaye hakuonekana kama mgombea mkuu Peter Kuwani anasemekana kujiapatia asilimia 2 ya kura hizo.

Mwaka uliopita, Malawi ilikuwa nchi ya pili barani Afrika kufutilia mbali matokeo ya uchaguzi wa urais kufuatia madai ya udanganyifu, baada ya Kenya 2017.

Mwandishi wa BBC katika eneo la kusini mwa Afrika, Andrew Harding anasema sio jambo la kawaida na kwa wengi linavutia - Mahakama iliingilia kati na kubadilisha matokeo katika eneo ambalo wizi wa kura ni suala la nyeti.