Naibu Waziri wa TAMISEMI Mwita Waitara, amesema kuwa mpaka sasa hivi amekwishamaliza kazi kubwa ndani ya Jiji la Dar es Salaam ya kukisambaratisha Chama cha CHADEMA, na kwa sasa  ameweka wazi kwa mara nyingine kuwa atakwenda kugombea ubunge katika jimbo la Tarime Vijijini mkoani Mara kupitia chama hicho.

Waitara amesisitiza kuwa haondoki Ukonga kwa sababu anamkimbia mtu, bali amekamilisha kazi ya kukisambaratisha Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), hivyo anakwenda Tarime Vijijini ambako ndipo anapotokea, kufanya kazi hiyo.

“Wala hakuna mtu ninayemkimbia, jimbo langu [Ukonga] lipo salama ndani na nje ya chama. Nimeshafanya kazi ya kuwasambaratisha CHADEMA hapa wameshapoteana. Walikuwa na Meya wa Jiji, hayupo, walikuwa na Meya Ilala, hayupo, walikuwa na Meya wa Ubungo, hayupo. Nishamaliza kazi Dar es Salaam, naenda kukamilisha kazi sehemu nyingine,” amesema Waitara.

Kiongozi huyo ambaye alihamia CCM akitokea CHADEMA Julai 2018 amesema kuwa Julai 14 mwaka huu atachukua fomu ya kuomba kuteuliwa kugombea ubunge Jimbo la Tarime Vijijini, na kwamba suala hilo sio siri.