SALVATORY NTANDU
Mbunge wa Jimbo la Kishapu mkoani Shinyanga Suleiman Masoud Nchambi (CCM) anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma ya kumiliki  silaha 10,risasi 536 na nyama zinazodhaniwa ni  za wanyamapori kilo 35  kinyume na sheria.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Shinyanga (ACP) Debora Magiligimba amethibitisha kukamatwa kwa Mbunge huyo na kusema kuwa tukio hilo limetokea Mei 3 mwaka huu majira ya saa sita usiku katika mtaa wa Lubaga Manispaa ya Shinyanga.

Amesema kuwa Jeshi la Polisi lilifanikiwa kukamata silaha hizo baada ya kufanya upekuzi  katika nyumba yake na baaada ya kupata taarifa za kiintelijensia kuwa Mbunge huyu anajihusisha na uwindaji haramu katika eneo la Negezi kwa kutumia gari lake aina ya Nisan hard body lenye namba za usajili T 760 DSD.

“Katika gari hilo kulikuwa na silaha moja aina ya shortgun ambapo baada ya kufanyika kwa ukaguzi katika chumba chake cha kulala zilipatikana silaha zingine 16,ambazo ni shortgun 3 Rifle 8,Pistol 1,Mark IV 1 pamoja na risasi hizo 536,”alisema Magiligimba.

Amefafanua kuwa Nyama hizo zimepelekwa katika maabara ya mkemia mkuu wa Serikali kwa uchunguzi na gari hilo limekamatwa na Mtuhumia atafikishwa Mahakamani baada ya upelelezi kukamilika.

Sambamba na hilo Magiligimba ametoa onyo kali kwa  mtu yeyote atakayebainika kujihusisha na vitendo vya kumiliki silaha bila kibali kwani hatua kali  za kisheria zitachukuliwa dhidi yake.

Mwisho