Zaidi ya watu 5,000 wamefariki dunia nchini Marekani kwa sababu ya janga la Corona, ambapo zaidi ya watu 215,000 nchini hump wameambukizwa virusi hivyo, Chuo Kikuu cha Johns-Hopkins kimetangaza, shirika la habari la AFP limeandika.

Hii ni baada ya watu 884   kuripotiwa kufariki dunia katika masaa 24, japo idadi hiyo ya Marekani ni ya chini ikilinganishwa na Italia na uhispania wakati huu maafa zaidi yakitrajiwa.

Wakati huo huo rais wa Marekani Donald Trump ametangaza kwamba anatathmini juu ya uwezekano wa kusitisha safari za ndege za ndani katika miji ya Marekani iliyoathiriwa zaidi na janga la Covid-19 (Corona), ambalo linaweza kuua watu wasiopungua 100,000 nchini humo, kulingana na ripoti ya mamlaka ya afya ya nchini Marekani.

"Tunatatmini hili, lakini mara tu hatua kama hiyo itakapochukuliwa, tutakuwa tumefunga sekta ambayo ni muhimu sana," Rais wa Marekani amesema wakati wa mkutano na waandishi wa habari huko Ikulu ya White House.

Jumanne wiki hii Donald Trump alionya, siku mbili baada ya kuongeza hatua za kuangamiza janga la Corona hadi mwisho wa mwezi wa Aprili, kwamba wiki mbili "mbaya zaidi" zinatarajia kushuhudiwa nchini Marekani katika vita dhidi ya ugonjwa huo.