Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa wa Songwe imeanza utekelezaji wa agizo la Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli la kuwataka wasafiri waliotoka katika nchi zenye maambukizi ya Virusi vya Corona kukaa karantini kwa muda wa siku 14 kwa gharama zao.

Jana wajumbe wa Kamati hiyo wametembelea eneo la mpaka wa Tanzania na Zambia uliopo eneo la Tunduma Mkoani Songwe ili kutathmini utayari wa kuanza zoezi la kuwaweka eneo tengefu yaani karantini wasafiri wote watakaotumia mpaka huo unao julikana kwa kuwa na watumiaji wengi zaidi nchini kutoka nchi mbalimbali.

Wajumbe hao wamekubaliana kuanza mara moja zoezi la kuwatenga wasafiri wote watakaoingia nchini kupitia Mpaka wa Tunduma kwa gharama zao na kwa muda wa siku 14, ambapo zoezi hilo lilitarajiwa kuanza jana Machi 23, 2020 usiku huku maandalizi ya maeneo na mahitaji mengine kwaajili ya kuwatenga yakiendelea kufanyika.

Pia wameweka mkakati wa kufanya kaguzi mbalimbali katika nyumba za kulala wageni ili kubaini endapo kuna wageni ambao wataingia nchini kwa kutumia njia zisizo halali na kukwepa kukaa karantini huku ulinzi ukiimarishwa Zaidi katika eneo lote la Mpaka.

Aidha wamewasihi wananchi wote kuendelea kuchukua hatua za tahadhari ili kujikinga na ugonjwa huo ikiwa ni pamoja na kunawa kwa maji na sabuni, kujiepusha na mikusanyiko isiyo ya lazima kwani kinga ni bora Zaidi kuliko Tiba.