Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi,-James Mbatia amevishauri vyama vya siasa nchini kusitisha mipango ya kuendesha mikutano ya hadhara, ili kupunguza tishio la kusambaa kwa virusi vya corona.

Mbatia ametoa ushauri huo jijini Dar es salaam, ikiwa ni siku moja baada ya serikali  kutangaza rasmi kuingia kwa virusi hivyo nchini.

“Kuhusu mikusanyiko, hili ni suala la utaifa, mikusanyiko isiyokuwa na kinga, haijalishi watu mia tano, watu mia mbili inabidi tuchukue tahadhari sana,” amesema Mbatia.

Ameishauri serikali kuhakikisha inatoa mwongozo na taarifa mara kwa mara kuhusu hali ya virusi hivyo pamoja na kuongeza elimu ya uraia kwa raia wanaoendelea kukusanyika.

Mbatia ambaye ni Mbunge wa jimbo la Vunjo mkoani Kilimanjaro amesema kuwa, tayari ameanza kuchukua tahadhari hiyo baada ya kusitisha ziara yake machi 21 mwaka huu katika kata 16 za jimbo hilo.