Afisa Habari wa klabu ya Yanga, Antonio Nugaz amezungumzia video inayosambaa mtandaoni, ikimuonesha akiwa katika sintofahamu na mashabiki baada ya mchezo wa ligi kuu dhidi ya Coastal Union, jana Februari 23.


Nugaz alikuwa katika sintofahamu na moja ya mashabiki wa klabu ya Coastal Union kufuatia kitendo chake cha kutaka kumrekodi bila ya ridhaa yake mara baada ya mchezo huo kumalizika kwa sare ya bila kufungana.

"Historia ya mashabiki hapa Tanga ni ustaarabu na ukarimu, lakini inapofikia kitendo cha mtu kuleta ujanja ujanja kutaka kurekodi bila ya ridhaa yangu na kutaka kutaka kunipora simu yangu ndiyo maana nikawa katika hali ile", amesema Nugaz.

"Yule hawezi kuwa mwananchi, hawezi kuwa Yanga mtu kama yule, sisi kawaida hatuna mambo kama yale. Hayo yameshapita, sasahivi kikosi kimeshawasiri Dar es Salaam kwa ajili ya maandalizi dhidi ya Gwambina FC katika mchezo wa Kombe la Shirikisho", ameongeza.

Yanga imeendeleza rekodi ya kutoshinda katika mechi za hivi karibuni, baada ya kupata sare katika michezo minne mfululizo ya ligi ambapo mpaka sasa imesalia katika nafasi ya nne ya msimamo, ikiwa na pointi 41.

Nafasi ya tatu inashikiliwa na Namungo FC yenye pointi 43 huku nafasi ya pili ikiwa chini ya Azam FC yenye pointi 45 na kinara Simba akiwa na pointi 62.