KAMA ulikuwa unadhani warembo wa Bongo pekee ndiyo wamefyatuka, basi unajidanganya kwa sababu kuna fyatu zaidi yao, Risasi Mchanganyiko lina habari ya tofauti.



NI ZODWA WABANTU

Miongoni mwa habari zilizoshtua wengi na kuibua gumzo barani Afrika hivi karibuni ni ya mrembo ambaye ni msanii, mnenguaji, modo, mwigizaji na video queen (muuza sura kwenye video), mwenye umaarufu zaidi mitandaoni (socialite) wa nchini Afrika Kusini ‘Sauzi’, Zodwa Rebecca Libram Wabantu.



AMILIKI JENEZA MIL. 22

Zodwa mwenye umri wa miaka 34 ambaye anajulikana kwa kusababisha matukio huku akiwa na umbo matata (hasa sehemu za nyuma) na kutoona aibu kukaa utupu, ndani kwake nchini Afrika Kusini anamiliki jeneza alilojinunulia la zaidi ya shilingi milioni 22 za Kibongo.

KWA NINI?

Kwa mujibu wa Zodwa, anajiandaa kwa kifo chake ili atakapokutwa na umauti, basi asiwape watu shida ya kuanza kutafuta jeneza la kumzikia.



Taarifa hizo zilieleza kuwa, Zodwa alilinunua jeneza hilo miezi kadhaa iliyopita ambapo lilimgharimu kiasi cha shilingi milioni moja za Kenya (zaidi ya shilingi bilioni 22 za Kitanzania).



Tukio hilo liliwashangaza maelfu ya wafuasi wake mitandaoni baada ya kujinunulia jeneza hilo la kifahari kwa ajili ya kujiandaa kwa mazishi yake. Kwa mujibu wa Zodwa, mwenyewe alipata taabu mno wakati wa kuchagua jeneza linalomfaa.



Hata hivyo, Zodwa aliwaeleza wafuasi wake zaidi ya laki tisa mitandaoni kwamba alifanya uamuzi huo kwa sababu hataki kifo chake kiisumbue familia yake na kuanza kuhangaika jinsi itakavyomzika. Katika maelezo yake, Zodwa alisema anataka kila tukio kwenye mazishi yake liendeshwe kwa utaratibu bila tatizo lolote.

LAZIMA UJIULIZE

“Lazima mtu ujiulize, hivi umejiandaa ipasavyo au unataka familia yako ihangaike wakati umeaga dunia? “Mimi sitaki nikifa watu waseme eti nilikuwa mtu maarufu na pesa nyingi, lakini hakuna pesa ya kugharamia mazishi..,” alisema Zodwa.



AONEKANA AKIJIPIMA

Kwa mujibu wa video za tukio hilo, Zodwa anaonekana akijipima kwenye jeneza hilo baada ya kulinunua. Kufuatia tukio hilo, wafuasi wake walionekana kushangazwa huku wengi wakijiuliza ni vipi mrembo huyo haofii kifo wala madhara ya kujipima kwenye jeneza.



GUMZO KAMA LOTE

Baadhi ya Wabongo walionesha kupigwa na butwaa juu ya tukio hilo huku wakitofautiana kimawazo na kuibua gumzo kama lote mitandaoni; “Amefanya jambo la maana sana kwa sababu hakuna ambaye hajui kuwa atakufa, ila tu je, ni lini? Au saa ngapi? Najua waoga wa kufa watampinga kwa alichofanya, lakini mimi naona yupo sahihi,” alichangia Mohammed.

“Hajakosea, yupo sahihi kabisa, anajua siku hizi maisha ni mafupi hasa pale anapokumbuka umauti na kuona wenzake wanakufa, anakuwa na hofu,” alichangia Binti Shamte. “Ajiandae kwa ibada na siyo jeneza kwa sababu unaweza ukaandaa jeneza ukafa, usionekane umefia wapi,” aliandika Aloyce.



ANAKUFA MUDA WOWOTE?

“Ni sawa kabisa, acha ajiandae maana kifo ndicho kilichobakia tu…” alichangia Ritha na kuongeza; “Ukiona hivyo ujue kuna kitu mtu ameona kwenye maisha yake, hivyo anaamini atakufa muda wowote.”



ZODWA NI NANI?

Zodwa ni mrembo maarufu barani Afrika kutokana na ushiriki wake kwenye sanaa hasa video za kucheza muziki majukwaani bila ‘kufuli’ (nguo ya ndani) ndani na nje ya Afrika Kusini.

DAVIDO AMTAKA

Miezi kadhaa iliyopita, staa wa muziki kutoka nchini Nigeria, David Adedeji Adeleke ‘Davido’ alieleza dhamira yake ya kumtaka Zodwa kufanya naye kazi kutokana na umaarufu wake barani Afrika.



MUGABE ALIMPIGA MARUFUKU

Mwaka 2017, aliyekuwa Rais wa Zimbabwe, Hayati Robert Mugabe aliwahi kupiga marufuku mrembo huyo kuingia nchini Zimbabwe. Mugabe alimpiga marufuku Zodwa kutokana na tabia yake ya kupanda jukwaani bila kuvaa nguo ya ndani.


Mugabe aliwaomba radhi wanaume ambao alidai kuwa amesikia wakilalamika kuhusu uamuzi huo. “Hatutaki mtu yeyote msumbufu kuja nchini kwetu akiwa mtupu kwa ajili ya kusababisha matatizo.


“Nini hasa lengo lake la kuja hapa?” Mugabe alihoji na kuongeza; “Ili wanaume waweze kukuona? Poleni. Tumewaangusha wanaume wengi ambao walikuwa wanalalamika. Nimesikia walikuwa wanataka Zodwa aje. Hayo ni mawazo ambayo hatuyataki, acha hayo yafanyike huko anakotoka (Afrika Kusini).”