Watu wanne wanaodhaniwa kuwa ni majambazi, wamefariki Dunia wakati wakijibizana risasi na Jeshi la Polisi katika eneo la Pori la Ngazi Saba, lililoko wilayani Biharamulo mkoani Kagera.


Kwa mujibu wa Kamishna wa Operesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi Liberatus Sabas, amesema tukio hilo limetokea wakati Polisi wakiwa katika Doria yao ya kawaida, ambapo waliona kundi la watu wakitokea katika pori hilo na kuwaamuru kujisalimisha.

Kamanda Sabas amesema badala ya kutii amri, watu hao waliwarushia Polisi risasi na polisi walipojibu walifanikiwa kuwapiga risasi na kupelekea vifo hivyo.

Kamishna huyo amesema kuwa Polisi kwa sasa wanaendesha operesheni maalum katika Mikoa ya Geita, Kigoma na Kagera, kufuatia mikoa hiyo kuwa na matukio mengi ya unyang’anyi wa kutumia silaha.