Msanii wa muziki nchini Tanzania, Diamond Platinumz amewataka wasanii wenzake kutokubali kuchonganishwa na kugombanishwa jambo ambalo halina tija kwa sanaa.

Kauli hiyo ya Diamond imekuja baada ya kuwashukuru wasanii wenzake wa ndani na nje ya Tanzania walioshiriki Wasafi Festival kwa kuleta mapinduzi katika tasania ya burudani nchini humo.

Amesema kwa muda mrefu kumekuwa na dhana ya ugomvi lakini tamasha la Wasafi lililohitimishwa jijini Dar es Salaam Jumamosi iliyopita Novemba 9, 2019 limekwenda kufuta dosari hiyo.

“Zamani kulikuwa na mambo ya uchonganishi, tulikuwa hatuendi kwenye shoo za wenzetu. Kupitia wasafi festival tumeifuta hiyo na nyie mkiwa na shughuli zenu nialikeni, tunavyojiweka mbali ndio tunatengenezewa maneno ya uchonganishi.” 
“Tunachonganishwa vitu vya uwongo na kweli tunachukiana wakati kila mtu ana mafanikio yake katika sehemu yake,” amesema Diamond