Polisi nchini Nigeria wamegundua zaidi ya vijana 70 wakiwa wamefungwa katika shule binafsi ya kiislamu huko kaskazini mwa Nigeria.

Mamia ya vijana wametoroka katika shule mbalimbali za dini ya kiislamu katika siku za hivi karibuni.

Shule za bweni za kiislamu zinazojulikana kama Almajiris ni maarufu sana kwa waislamu wengi kaskazini mwa Nigeria.


Wazazi wanaowapeleka watoto wao katika shule hizo huwa wana matumaini ya kuwarekebisha tabia watoto wao kwa kupata elimu ya dini ya kiislamu.

Ingawa baadhi ya vijana waliookolewa katika vyuo hivyo wanadai kuteswa na kunyanyaswa kingono.

Rabiu Umar Galadima mwenye miaka 26 ni miongoni mwa vijana waliookolewa katika moja ya shule hizo huko mji wa Daura, eneo ambalo rais wa taifa hilo Muhammadu Buhari ametokea.

Galadima ameiambia BBC kuwa walikuwa wanatunzwa kama wanyama.

"Nilikuwa nachapwa fimbo 10 asubuhi, 10 mchana na jioni pia fimbo kumi, Nilikuwa nateswa, napigwa,nilikuwa kama mnyama",

Walimu wawili na mmiliki shule hiyo, mjini Daura, ambapo ndipo Rais Muhammadu Buhari amezaliwa, wamekamatwa.