Eric Msuya – MAELEZO.

Naibu waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Stellah Manyanya amewataka wadau wa Sekta hiyo kutumia mfumo mpya wa kukusanya Taarirfa za Kibiashara Nchini kwa lengo la kupiga hatua kuelekea Tanzania ya Viwanda na Uchumi wa kati.

Kuanzishwa kwa mfumo huo ujulikanao kama Trade Information Module, ni utekelezaji wa makubaliano ya kimataifa yaliyopo kwenye mkataba wa uwezashaji wa Kibiashara unaosimamiwa na Shirika la Biashara Duniani.

Manyanya aliyasema hayo jana, Jijini Dar es Salaam katika mkutano wa Wafanyabaishara na Wadau wa Biashara, kuhusu mfumo wa utoaji wa Taarifa za Kibiashara Nchini, ambapo alisema, mfumo huo mpya utasaidia utunzanzaji na upatikanaji wa taarifa za Leseni pamoja na Vibali mbalimbali vya kufanyia Biashara Nchini.

“kama manavyojua, upatikanaji wa Taarifa ni muhimu sana katika kufanya maaamuzi ya kila jambo hivyo uwepo wa Taarifa hizi za Biashara mahali pamoja utasaidia Wafanyabiashara kujua mahitaji, utaratibu na mahali pa kupata vibali mbalimbali” alisema Mhe. Stellah.

Alisema mfumo huu utaliwezesha Taifa kupata Fedha za kigeni sambamba na kumsaidia mfanyabiashara kujua taratibu na masharti ya kuingiza Bidhaa zao Nchini kupitia Masoko ya Nje ya Nchi.

Sambamba na hilo, Mhe. Stellah aliwataka Wafanyabiashara na Wadau mbalimbali kutumia mfumo huo vizuri kwani utaleta Mapinduzi makubwa katika Sekta ya Biashara Nchini pamoja na kuondoa kero mbalimbali.

“lakini pia mfumo huu utaongeza ukaribu baina ya Wafanyabaishara na Ofisi za Umma, utaongeza ufanisi na kupunguza gharama za Kibiashara, utapunguza muda anaotumia Mfanyabiashara kupata Leseni, hivyo kwa ujumla mfumo huu utaboresha Mazingira ya Kibiashara Nchini kwa kuchangia Uchumi wa Nchi” alisema Mhe Stellah.

Pamoja na hilo, Serikali ya awamu ya Tano, kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara, inaendelea kufanya jitihada mbalimbali za za kuboresha Mazingira ya Kibiashara Nchini (Blueprint For Regulatory Reform to Improve Business Environment) ili kuweza kuwavutia wawekezaji wa ndani na Nje ya Nchi kuja kuwekeza hapa kiurahisi.

“tunafanya jitihada nyingi sana ili kuboresha mazingira nchini hususan mfumo wa udhibiti wa biashara Tanzania” alisema Manyanya.