Na Veronica Simba – Tanga
Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), itatoa vyeti maalum kwa wakandarasi wa miradi ya umeme vijijini, watakaokamilisha kazi kwa wakati na viwango stahiki, ili kuwapa motisha na utambuzi utakaowapa sifa ya kupewa tenda nyingine mbalimbali na Serikali.

Hayo yalibainishwa Oktoba 22, 2019 jijini Tanga, na Mwenyekiti wa Kamati ya Ufundi ya Bodi ya Wakurugenzi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REB), Mhandisi Styden Rwebangila, akiwa katika ziara ya kazi kukagua utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini, mkoani humo.

Mhandisi Rwebangila ambaye aliambatana na wajumbe kadhaa wa Bodi husika pamoja na wataalamu kutoka Wakala huo, alisema baada ya kukagua magenge na ghala la vifaa vya Mkandarasi Derm Electrics (T) Ltd katika wilaya za Handeni, Korogwe, Kilindi na Lushoto, wameridhishwa na kazi yake lakini wakamtaka asibweteke bali aendeleze jitihada ili akamilishe kazi kwa wakati.

“Kama akiendelea hivi, basi atakuwa ni miongoni mwa watakaopata vyeti maalum vya utambuzi kutoka REA,” alisema Rwebangila.

Naye Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Ufundi kutoka REA, Mhandisi Jones Olotu, ametoa wito kwa wakandarasi wote 16 wanaotekeleza miradi ya umeme vijijini, awamu ya tatu, mzunguko wa kwanza, kuhakikisha wanawaunganishia umeme wateja katika maeneo yao wakiwemo wale wasio na uwezo wa kugharamia utandazaji mfumo wa nyaya katika nyumba zao.

Olotu alisema, siyo lazima mwananchi afunge mfumo wa nyaya ili kuunganishiwa umeme kwani kuna njia mbadala ya kutumia kifaa cha Umeme Tayari (UMETA), ambavyo kila Mkandarasi amepatiwa 250 kwa kila eneo analotekeleza kazi kwa ajili ya kuwafungia wananchi wenye uhitaji.

“Natoa wito kwa wakandarasi wote husika; Mteja yeyote ambaye yuko ndani ya wigo, kama hajafanya ‘wiring’, afungiwe UMETA, awekewe balbu tatu na ashauriwe kufanya ‘wiring’ taratibu. Atakapokamilisha, atabadilishiwa mfumo,” alisisitiza.

Kamati hiyo ya Ufundi ya Bodi ya REA, imeanza mzunguko wa pili wa ziara ya kutembelea maeneo mbalimbali inakotekelezwa miradi ya umeme vijijini, hususan mahali ambako utekelezaji unasuasua, ili kujua kulikoni pamoja na kutafuta ufumbuzi wake.
 Mwenyekiti wa Kamati ya Ufundi ya Bodi ya Wakala wa Nishati Vijijini (REB), Mhandisi Styden Rwebangila (kushoto), akikagua moja ya transfoma katika ghala la Mkandarasi Derm Electrics (T) Ltd, anayetekeleza mradi wa umeme vijijini mkoani Tanga. Wa pili kutoka kulia ni Mjumbe wa Bodi hiyo, Louis Accaro na kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Ufundi kutoka REA, Mhandisi Jones Olotu. Timu hiyo ilikuwa ziarani mkoani Tanga, Oktoba 22, 2019.


 Matukio mbalimbali wakati Kamati ya Ufundi ya Bodi ya Wakurugenzi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REB), ilipofanya ziara katika Wilaya mbalimbali za Mkoa wa Tanga, Oktoba 22, 2019, kukagua utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini.