DAR ES SLAAM: Bado upepo siyo mzuri ndani ya Lebo ya Wasafi Classic Baby (WCB)! Siku chache baada ya mwanamuziki wake, Rajab Abdul Kahali ‘Harmonize’ kujitoa kwenye lebo hiyo, imebainika pia meneja wa mwanamuziki Mbwana Yusuph Kilungi ‘Mbosso’, Almah Bronxi naye amefungasha virago vyake, Gazeti la Ijumaa Wikienda linao ubuyu kama wote!



CHUKUA HII KWANZA

Kama ulikuwa hujui, Almah alipokea kijiti cha umeneja wa Mbosso tangu Julai, mwaka huu baada ya aliyekuwa meneja wa mwanamuziki huyo, Sandra Brown kubwaga manyanga.

Sandra naye aliitumikia nafasi hiyo kwa takriban mwaka mmoja, akasepa zake kwa kile kilichodaiwa kuwa ni kutoenda sawa kuhusu maslahi na uongozi wa WCB.



TUREJEE KWENYE UBUYU WETU

Kwa mujibu wa chanzo makini cha kuaminika, meneja huyo ameamua kubwaga mzigo baada ya uongozi wa WCB kumtaka atumikie kwa asilimia mia moja lebo hiyo na asiipe nafasi kampuni yake ya burudani iitwayo Bronxi Entertainment.



MENEJA AGOMA

Imeelezwa kuwa, meneja huyo alikataa kuitumikia Wasafi asilimia mia moja kwani kwa kufanya hivyo kungeua ‘brand’ yake ya Bronxi Entertainment inayowasimamia pia wasanii maarufu Afrika akiwemo Patoranking wa Nigeria.



Mbali na brand hiyo kuwa maarufu, imeelezwa kuwa meneja huyo hakuwa tayari kuiua kampuni yake hiyo ambayo ameijenga kwa takriban miaka sita iliyopita.

“Wiki chache zilizopita, Bronxi kupitia kampuni yake, aliisimamia kwa mafanikio makubwa sana ziara ya msanii kutoka Nigeria, Seyi Shay kutua nchini Tanzania, hivyo mabosi wa Wasafi walipoona hivyo hawakufurahishwa, wakamueleza kuwa adili na Wasafi pekee na kama hawezi, basi asepe,” kilisema chanzo makini.



WASAFI WAMKANA

Mara baada ya ubuyu huo wa moto moto kumwagika kama wote, mmoja wa mameneja wa Wasafi, Sallam SK Mendez alimkana meneja huyo na kusema hawakuwa na mkataba naye.

“Bronxi hatukuwa na mkataba naye kama meneja wa Mbosso. Ingekuwa ni hivyo tungetangaza kwa umma. Yeye alichokuwa anakifanya alikuwa ni mtu wa kusimamia shoo za nje ya nchi za Mbosso ambapo pia hakufanya hivyo,” alisema Mendez na kuongeza;


“Najua alikuwa anatumia mitandao yake ya kijamii kutangaza kuwa ni meneja mpya wa Mbosso, lakini ukweli ni kwamba hakuwa.”



MAONI YA WADAU Baada ya ubuyu huo kutua kwenye Gazeti la Ijumaa Wikienda lilijaribu kuzungumza na wadau mbalimbali wa burudani Bongo ambao walionesha kushtushwa na taarifa hizo na kuhoji kunani Wasafi?



“Mh! Jamani kutakuwa na nini hapo Wasafi? Si juzijuzi tu hapa Harmonize ametoka? Mara tena meneja wa Mbosso naye ameondoka? Kuna kitu hapo, inabidi ninyi kama waandishi muendelee kuchimba zaidi ili kubaini ukweli zaidi,” alisema Leornad Mutabuzi, mkazi wa Mbezi-Beach, jirani na ofisi za Wasafi jijini Dar.



Mbali na huyo, Ijumaa Wikienda pia lilipokea maoni kutoka kwa mkazi mwingine wa Sinza jijini Dar, Emmanuel Edson ambapo alipoelezwa kuhusu taarifa za meneja huyo kuondoka WCB, alisema ni taarifa inayofikirisha na kuanza kupata shaka nani atafuatia.

“Unajua juzi tu hapa ameondoka Harmonize, leo unaniambia tena meneja wa Mbosso naye anaondoka, sasa huoni kwamba hapo kuna taa nyekundu inawaka? Unajiuliza who is next? (nani atafuata)” alihoji Emmanuel.



MFUMO WA WCB

Mfumo wa uongozi wa WCB, umeweka utaratibu wa kila msanii ambaye yupo kwenye lebo hiyo kuwa na meneja wake binafsi. Mameneja hao binafsi wanatakiwa kuripoti kazi zao kwa uongozi wa juu ambao unaongozwa na Diamond, Sallam, Babu Tale na Said Fella.

Stori: Erick Evarist