Mwanyekiti wa Bodi ya TGNP Mtandao, Aseny Muro akimkabidhi Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Dkt. Bashiru Ally, Nakala ya Ilani ya madai ya wanawake katika uchaguzi wa serikali za Mita 2019 na uchaguzi Mkuu 2020 leo katika Ofisi ndogo ya CCM Lumumba Dar es salaam, Anayefuatia ni Mkurugenzi Mtenaji wa TGNP, Lilian Liundi.

Na Deogratius Temba.

Katibu mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Dkt Bashiru Ally, ameyataka mashirika yanayotetea haki za wanawake na usawa wa Kijinsia kutoa elimu kwa jamii juu ya umuhimu wa ushiriki wa wanawake katika nafasi za maamuzi ngazi ya jamii ili kulinda rasilimali za umma na kuhakikisha zinawanuafaisha wananchi wote.

Akizungumza wakati wa kikao kifupi cha TGNP na CCM makao makuu kilichokuwa na lengo la kukabidhi Ilani ya madai ya wanawake katika Uchaguzi wa serikali za Mitaa 2019 na Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020, Dkt bashiru alisema kwamba, TGNP Mtandao imefanya kazi kubwa ya kuhakikisha jamii inapata uelewa wa kudumu juu ya haki zao na uwajibikaji wa wananchi katika kulinda, kutunza na kuendeleza rasilimali zao.

“ Ninajua jinsi ambavyo TGNP Mtandao, imejikita katika kujenga uelewa kwa wananchi, mifumo na mbinu mnazotumia kufikia wananchi ni mizuri, ninajiuliza tu, nchi hii ni kubwa ni namna gani mtaweza kufikia watu wengi zaidi? Je mnazo rasilimali za kufika kila mahali? Mbinu zinazotumika kutoa mafunzo zinaweza kuwafikia wote? Au tubadilishe mbinu? “ alisema Dkt Bashiru

Alisema kwamba TGNP na asasi zingine za kiraia ni muhimu kuendelea kuweka nguvu katika kuelemisha jamii, kujenga uwezo kwa wananwake kuwa viongozi wazuri, kufikia mifumo yote ya kijamii na kiseirkali ili kuhakikisha tunakuwa na taifa linalojali na kuheshimu masuala ya usawa wa kijinsia katika Nyanja zote.

Alisisitiza kuwa. “TGNP na wengine, jengeni uwezo kwa kamati muhimu ambazo wanaawake wanaziongoza, mifumo mizuri inayowagusa watu ni ile iliyoko chini kabisa kwenye jamii, mfano, kamati ya maji, ardhi, mazingira… waelimisheni vizuri na kama kuna wanawake wameshika nafasi humo waoneshe mabadiliko ya haraka, jamii inaheshimu na kuona kwamba kuna umuhimu wa wanawake kushika nafasi za maamuzi”

Naye Mwenyekiti wa TGNP Mtandao, Aseny Muro, alimshukuru katibu Mkuu kwa kazi nzuri na kumshukuru Mwenyekiti wa CCM Taifa Dkt. John Magufuli kwa kuendelea kulinda na kutetea rasilimali za taifa ambazo nyingi zinawanufaisha wanawake na watoto ikiwepo kuboresha huduma za jamii.

Ilani ya madai ya wanawake katika uchaguzi wa serikali za Mitaa 2019 na uchaguzi Mkuu 2020, imeandaliwa na Mtandao wa Wanawake na Katiba na uongozi na Mfuko wa Wanawake Tanzania (WFT).