Baada Ijumaa kukusanya Sh. mil 10.8 kwenye harambee ya kuichangia Yanga iliyofanyika jijini hapa sasa inakuja na kishindo kingine cha udhamini ambao utatikisa na kurejesha klabu hiyo kwenye hadhi yake.

Mwenyekiti wa Yanga, Dk Mshindo Msolla ameweka wazi pia kwamba kila mwezi wanatumia Sh.Mil 300 kulipa mishahara na Sh.Mil 200 kwenye gharama za uendeshaji.

Yanga wametamba kwamba ujio wa udhamini huo wa mamilioni kutoka kwenye kampuni hiyo ya nje ya Tanzania kutaisaidia klabu kukabiliana na ushindani wa Simba, wenye kiburi cha bilionea mzalendo Mohammed Dewji ‘MO’.

Msolla ambaye ndiye kiongozi msomi zaidi katika klabu za Ligi Kuu Bara msimu huu, licha ya kutotaja jina la kampuni hiyo lakini amesema udhamini wake utagharimu zaidi ya bilioni moja kwa mkataba wa mwaka.

“Naomba nitamke wazi mbele yenu kwamba tuko njiani kupata mdhamini atakayekuwa akitoa pesa zaidi ya SportPesa kwani yeye atakuwa akitoa zaidi ya bilioni moja za Kitanzania na tayari tumesaini mkataba wa makubaliano ya awali na mazungumzo yanaendelea,” alisema Msolla ambaye amewahi kuwa Kocha wa Taifa Stars na Reli ya Morogoro.

“Kutokana na makubaliano yalivyo huyu mdhamini ataanza kutudhamini kuanzia msimu ujao na mambo yakienda kama tulivyopanga kuanzia mwezi Januari tutaanza kuingiziwa kwenye akaunti yetu milioni themanini mpaka ligi
itakapomalizika na yeye atakuwa mdhamini wetu kwa msimu ujao wa ligi.

“Mpaka sasa uongozi wetu umekaa miezi minne tu madarakani lakini kuendesha timu ni gharama tunaamini kwa jinsi tunavyotengeneza mazingira ya kupata fedha kwa hakika shilingi Mil 300 tunazotumia kulipa mishahara na Mil 200 za uendeshaji kwa mwezi mmoja tutapata tiba yake kwa kuwa watu wengi wameonyesha nia ya kuja kuwekeza katika klabu yetu kwa kufuata utaratibu wa kisheria,” alisema Msolla.