Waziri Mbalawa Alipongeza Shirika La Maendeleo La Ujeruman Kwa Kufanikisha Mradi Wa Maji Ulioshindikana Takribani Miaka 7.SERIKALI imesema kuwa imejipanga kukarabati miradi yote ya maji iliyotelekezwa kwa kipindi kirefu ili kupunguza adha ya uhaba wa maji kwa wananchi.

Hayo yamebainishwa jana Septemba 11,2019  jijini Dodoma  na Waziri wa Maji Prof.Makame Mbalawa wakati akihutubia wananchi wa Kata ya Nghong'onha Katika hafla ya uzinduzi wa Mradi wa maji Katika kata hiyo .

Waziri Mbalawa amesema makandarasi wa ovyo wamekuwa wakikwamisha juhudi za serikali Katika maendeleo na kusababisha hasara hivyo  kuwataka kujitathimini upya.

"Serikali haitomfumbia macho mkandarasi yeyote anayegeuza miradi ya maji Kama kitega uchumi chake,lazima kila mtu akae kwenye mstari kuhakikisha anafanya maendeleo kwa moyo mmoja,"amesema.

WaziriProf.Mbalawa amesema Mradi wa maji Katika kata hiyo ulianza tangu  mwaka 2013  ambapo umechukua miaka 7 kukamilika kwake huku akilipongeza Shirika la Maendeleo la Ujeruman [ GIZ ]Kwa kufanikisha mradi huo.

"Huu ni uzembe mkubwa ,Mradi wa maji unachukua miaka mingi tunaweza kuufananisha na umri wa mtoto ambapo mwaka 2013 angezaliwa mwaka angeanza darasa la kwanza,"alisema na kuongeza,

"Katika Mradi huu kulifanyika uzembe wa hali ya juu na uhuni kwani Mradi huu ulitakiwa kukamilika kwa kipindi Cha miezi sita tu tangu kuanza kwake,"alisisitiza Mbalawa.

Kutokana na hayo amewataka watendaji wote wa wizara ya maji kuhakikisha wanakuwa makini kushughulikia miradi ya huduma za kijamii ili kuhakikisha inaondoa kero kwa wananchi.

Mwakilishi wa Shirika la maendeleo la Ujerumani (GIZ)Vera Rosender alisema Mradi huo Hadi kukamilika ,umegharimu jumla ya shilingi milioni 350 huku akiongeza kuwa Serikali ya Ujerumani kwa kuona umuhimu wa maendeleo iliamua kusaidia kuwapatia maji wakazi hao ambao tangu kipindi Cha Uhuru hawajawahi kuwa na maji ya uhakika.

Kwa upande wake mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya maji na usafi wa mazingira (DUWASA)Mhandisi David Palangyo aliishukuru serikali ya Ujerumani kujitolea kushirikiana nao kutatua kero ya maji kwa wakazi wa Kata ya Nghong'onha .

Mhandisi huyo amesema wao Kama wadau wa maji watahakikisha wanakuwa karibu na wakazi hao kuhakikisha wanalinda miundombinu ya maji huku wakijipanga kuanzisha kamati ya maji ya kata hiyo itakayosimamia mapato kwa uzalendo.

"Hakuna asiyefahamu shida nliokuwa mkiipata,na Sasa mmepata maji moiyoyatamani kwa kipindi kirefu tafadhalini ndugu zangu tushirikiane kwa pamoja kuyaenzi kwani maji ni uhai,"alisema.

Pia amefafanua kuwa  kabla ya Mradi huo kukamilika wananchi walikuwa wakitumia maji yasiyo salama na kwamba walinunua ndoo moja ya maji kwa shilingi miatano ambapo kwa Sasa Lita 20 ya maji itauzwa kwa shilingi 25.

Naye Kaimu mkuu wa mkoa wa Dodoma ,ambaye pia ni Mkuu wa  wilaya Patrobas Katambi aliwataka wananchi wa Nghong'onha kuitunza miundombinu ya maji na kuepuka kuihujumu.

"Tunafahamu Kuna watu hawapendi maendeleo nataka kuwaambia kila mtu awe mlinzi wa mwenzie ,hakikisheni pia mnalinda mazingira ya vyanzo vya maji ili kiendelea kufurahia  huduma hiyo,"amesema.

Mbunge wa Jimbo la Dodoma  Mjini ambaye pia ni Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu ,Kazi ,vijana na Ajira,Mhe.Anthony Mavunde amesema kukamilika kwa mradi huo itakuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi wa eneo hilo ambapo amebainisha kuwa alikuwa halali usiku na mchana kutafuta mwarobaini wa kutatua kero ya maji.
“Wakati nasaka kura hapa nilisema yasipokuja maji Nghong’ona  mpaka kufikia mwaka 2020 msinipigie kura,Moyo wangu ulikuwa unadunda sasa inakaribia 2020 na Maji bado,nililuwa silali napita hapa na pale kuhakikisha tatizo la uhaba wa maji linatatuliwa,lakini sasa imekuwa historia tujivunie tatizo hili ni la muda mrefu .amesema.

Kwa upande wao Baadhi ya Wananchi wa kata hiyo wamesema uzinduzi wa Mradi huo wa maji utawasaidia kuepukana na kero kubwa ya adha ya maji ya kutembea umbali mrefu kutafuta huduma hiyo ambapo awali ndoo moja walikuwa wananunua kwa Tsh.300 hadi 400 lakini sasa watakuwa wananunua kwa Tsh.25 tu kwa ndoo katika mradi huo hali ambayo itapunguza ukali wa Maisha.

 Jumla ya wakazi  10500 wa Kata ya Nghong'onha wanatarajiwa kunufaika na Mradi huo.