Papa Francis leo anaanza ziara rasmi ya kihotoria barani Afrika wiki hii - akiwa anazitembelea Msumbiji, Madagascar na Mauritius.

Umaskini, uhifadhi wa mazingira na ufisadi ni miongoni mwa mambo yanatorajiwa kuigubika ziara ya Papa katika mataifa ya Afrika.

Wahudumu katika kanisa katoliki wamenukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari wakisema kwamba ziara hii ambayo ni ya pili Papa Francis kuwahi kuifanya kusini mwa jangwa la Sahara Afrika, ni fursa muhimu kutoa wito mpya uliogubikwa katika barua yake ya mnamo 2015 "Laudato Si" inayuhusu kulinda mazingira.

Changamoto kubwa inayomkabili Papa kwa sasa
Papa Francis azungumzia mkasa wa pete yake
Katika mataifa ya Msumbiji na Madagascar kumeshuhudiwa pakubwa tatizo la ukataji miti.

Mambo ambayo pamoja na mmomonyoko wa udongo, yamechangia Msumbiji kuwa katika hatari wakati vimbunga viwili vilipotuwa katika taifa hili mwaka huu, linaripoti shirika la habari la Reuters.

Kwa mujibu wa takwimu za benki ya Dunia, Msumbiji imepoteza hekari milioni 8 za misitu - tangu katika miaka ya 70.

Masuala mengine yanayotarajiwa kuigubika ziara ya Papa katika mataifa hayo ya Afrika ni umasikini, vita na ufisadi au rushwa.

Katika mahojiano naVatican News, Kadinali Pietro Parolin, ambaye ni waziri wa mambo ya nje wa Vatican amesema Papa anatazamiwa kutuma ujumbe mzito kuhusu amani na majadiliano.

Licha ya kwamba baadhi hulihusisha bara la Afrika na matatizo kama mizozo na majanga, kadinali huyo anaamini kuwa "Afrika ni zaidi ya yote eneo lililo na utajiri wa utu au ubinaadamu, lenye utajiri wa maadili na imani", na kwamba anahisi Papa anafanya ziara hii akiwa pia na hisia kama hizi, inaripoti Vatican news.

Ziara hii ya Papa Francis inatazamwa kama jitihada zake ya kuwa na malengo mapya chini ya uongozi wake baada ya kashfa za miezi kadhaa kuhusu namna kesi za unyanyasaji wa kingono zilivyoshughulikiwa.

Papa Francis anaonekana kuwa na umakini wa kurudi katika kauli mbiu ya amani, utengamano na jitihada za kumaliza umaskini.

Ziara nyingine za Papa Mtakatifu Afrika
Mara ya mwisho Papa Francis kuizuru Afrika ilikuwa Novemba 25 mnamo 2015.

Alianza kwa kutua nchini Kenya akaelekea Uganda na kumalizia ziara hiyo katika Jamhuri ya Afrika ya Kati.

Watawa watumishwa kama watumwa wa ngono
Kwanini ziara ya Papa huko Arabuni ni muhimu ?
Katika ziara hiyo ya siku sita, Papa alieneza ujumbe wake wa Amani, maridhiano, mashauriano na kuchochea juhudi za kuzima migawanyiko.

Akiwa nchini Kenya, Papa Francis alisema: "Vijana ndio rasilimali yenye thamani zaidi kwa taifa. Kuwalinda, kuwekeza katika vijana, na kuwasaidia, ndiyo njia bora zaidi ya kuhakikisha siku njema za usoni zenye kufuata busara na maadili ya kiroho ya wazee wetu, maadili ambayo ndiyo nguzo ya jamii."

Papa alitumia Kiswahili kuhitimisha hotuba yake, akisema: "Mungu abariki Kenya!"

Alikuwa ameandika maneno yayo hayo kwenye akaunti yake ya mtandao wa kijamii wa Twitter alipokuwa safarini, saa moja hivi kabla ya kuwasili Kenya.

Kando na Papa Francis, Mapapa wawili wengine wamewahi kuzuru mataifa ya Afrika.

Wa kwanza alikuwa Papa Paul VI aliyezuru Uganda mwaka 1969.

Baadaye Mtakatifu John Paul II alizuru mataifa 42 ya Afrika akitembelea Kenya mwaka 1980, mwaka 1985 na mwaka 1995; Uganda mwaka 1993; na Jamhuri ya Afrika ya Kati 1975.