Polisi Mkoani Mara wanamshikilia Mwalimu Mkuu Msaidizi wa Shule ya Msingi Bwai A, Wilayani Musoma Lazaro Mmanga kwa tuhuma za kumbaka (ofisini) Mwanafunzi wa darasa la saba wa shule hiyo mwenye umri wa miaka 14 wakati akijiandaa kufanya mtihani wa Taifa.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, Juma Ndaki, alisema mwalimun huyo alimpitisha mwanafunzi  dirishani na kumuingiza ofisi ya mwalimu mkuu, kisha kufunga mlango wa kutokea nje na yeye kuzunguka dirishani, kisha kuingia ndani ya ofisi hiyo.

Alisema baadhi ya wanafunzi waliokuwa wakimwagilia maua pembeni waliona tukio hilo,kisha kutoa taarifa kwa viongozi wa kijiji na kumkamata mwalimu akiwa na mwanafunzi ofisini, kisha kumfikisha kituo cha polisi Mugango.

Kamanda Ndaki alisema baada ya kufikishwa kituoni, baadhi ya wananchi walivamia kituo hicho kwa lengo la kutaka kumuua na kutokea fujo zilizosababisha gari la polisi kupondwa mawe na kutaka kuchomwa moto, polisi walifanya jitihada za kukabiliana na vurugu hizo.

Alisema kutokana na vurugu hizo, watu 42 wanashikiliwa na polisi kutokana uharibifu wa mali.