Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amesema kuwa Wizara yake haijatangaza hali ya hatari juu ya ugonjwa wa Ebola bali wametoa tahadhari kwa Umma kuhusu tishio la ugonjwa huo.

Waziri Ummy amesema kuwa wametoa tahadhari ili wananchi wachukue tahadhari na kujikinga na kuhakikisha ugonjwa huu hauingii nchini.

"Ufafanuzi: Wizara ya Afya haijatangza hali ya hatari bali tumetoa tahadhari kwa Umma kuhusu Tishio la Ugonjwa wa Ebola ili wananchi wachukue hatua za kujikinga na kuhakikisha ugonjwa huu hauingii nchini kwetu," alieleza Waziri Ummy kwenye mitandao yake ya Kijamii.

"Ninawasihi wananchi kutokuwa na hofu kwani mpaka sasa hakuna mgonjwa yoyote alieripotiwa au kuhisiwa kuwa na dalili za Ebola hapa nchini. Muhimu tushirikiane kwa pamoja kuhakikisha ugonjwa huu hauingii nchini kwa kuzingatia maelekezo yaliyotolewa na yatakayoendelea kutolewa na @wizara_afyatz. Ninawasihi vyombo vya habari/wananchi kujiepusha na utoaji wa Taarifa ambazo si sahihi."