Na Issa Mtuwa – Dodoma
Waziri wa Madini Doto Biteko amekutana na Mwekezaji wa Kampuni ya Ngwena Tanzania Ltd “Ngwena” na kufanya nao mazungumzo kuhusu masuala mbalimbali, kubwa likiwa ni kutoa Ufafanuzi kuhusu Marekebisho ya Sheria ya Madini inavyotoa fursa na mazingira mazuri ya uwekezaji katika sekta ya madini hapa nchini.
 Hatua hiyo inafuatia ombi la kampuni hiyo kuomba kukutana na waziri Biteko ili kupata ufafanuzi wa moja kwa moja kutoka kwake kuhusu mabadiliko hayo ya sheria.

Ombi la kutaka kuonana na waziri ni kutokana na kampuni ya Ngwena kupata taarifa za upotoshaji na zisizo sahihi kuhusu mabadiliko ya sheria ya madini yaliyofanywa na Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu taratibu mbalimbali za uwekezaji na shuguli nyingine zinazo husu sekta ya madini.

Upotoshaji unaofanywa kwa maksudi na baadhi ya watu ndani nan je ya nchi kwa lengo la kutaka kuifanya Tanzania kama sio mahali sahihi pa kuwekeza. 
Biteko ameuambia ujumbe wa kampuni ya Ngwena kuwa, mabadiliko ya sheria yamefanyika kwa kuzingatia maslahi ya pande zote mbili mwekezaji na taifa kwa upande mwingine. 

Amefafanua kuwa, tangu mabadiliko hayo yapitishwe hakuna malalamiko ya kupingwa kwa marekebisho hayo kwakuwa yalizingatia maslahi mapana ya kila upande na kuhakikisha mazingira ya uwekezaji yanakuwa rafiki na ndio sababu mpaka sasa tangu marekebisho hayo yafanyike hakuna kampuni au muwekezaji alie acha wala kuonyesha nia ya kufunga shuguli zake kwa sababu ya marekebisho ya sheria.

Ameongeza kuwa, Tanzania inawahitaji sana wawekezaji na mara zote kila panapokuwa na jambo haliendi sawa mara moja hukaa na kujadili na mwekezaji na kutatua changamoto.
 Ameitaka kampuni ya Ngwena kwenda kuwa mabalozi ili kuwaeleza  wengine kuhusu ukweli ulivyo kuhusu marekebisho ya sheria yaliyofanywa na kuachana na upotoshwaji unaofanywa na baadhi ya watu ambao hawana dhamana ya kuyazungumzia masuala hayo. 

Amewakaribisha watu na wawekezaji wote wanaotaka kupata ufafanuzi wa jambo lolote kutembelea ofisini kwake jijini Dodoma.
Aidha, kwa upande wa kampuni ya  Ngwena ukiongozwa na Meneja Mkuu H.E Kavishe amemshukuru Waziri kwa ufafanuzi mzuri alioutoa na kwamba walichokuwa wanakisikia na alichokisema waziri ni vitu tofauti na kuongeza kuwa, kuonana kwao kumewafungua masikio na kupata ukweli kutoka kwenye mtu sahihi na mwenye dhamana ya sekta ya madini.

Ameongeza kuwa, ni kweli upotoshaji waliokuwa wanaupata ungeweza hata kuwarudisha nyuma, hivyo watakwenda kufikisha ujumbe kwa wenzao.
Kikao hicho pia, kimehudhuriwa na Katibu Mkuu Wizara ya Madini Prof. Simon Msanjila, Kamishna wa Madini, Mhandisi David Mulabwa, Mkurugenzi wa Huduma za Sheria Edwin Igenge, na Mkurugenzi wa Sera na Mipango  Wizara ya Madini, Augustine Ollal, Kamishna masaidizi anaeshuugulikia Migodi na Biashara Ali Ali na  Kamishna masaidizi anaeshugulikia Lesseni Maduh.
 Waziri wa Madini Doto Biteko wa Kulia katikati akisisitiza jambo wakati wa kikao chake na ujumbe wa Kampuni ya Ngwena Tanzania Ltd “Ngwena” waliomtembelea waziri kupata ufafanuzi kuhusu marekebisho ya sheria ya madini. Kulia kwake ni Katibu Mkuu wizara ya Madini Prof. Simon Msanjila.

 Waziri wa Madini Doto Biteko wa Kulia na Katibu Mkuu wizara ya Madini Prof. Simon Msanjila kushoto  katikati wakiwasikiliza wageni wao wakati wa kikao cha pamoja na ujumbe wa Kampuni ya Ngwena Tanzania Ltd “Ngwena” waliomtembelea waziri ofisini kwake kupata ufafanuzi kuhusu marekebisho ya sheria ya madini. 
Waziri wa Madini Doto Biteko hayupo pichani akimsikiliza kwa makini mmoja wa wajumbe wa Kampuni ya Ngwena Tanzania Ltd “Ngwena” waliomtembelea ofisini kwake kuja kupata ufafanuzi kuhusu marekebisho ya sheria ya madini.