Ikulu ya Urusi mjini Moscow imekanusha kauli ya rais wa Marekani Donald Trump, kwamba inapanga kuwaondoa wanajeshi wake kutoka Venezuela.

Kupitia ukurasa wake wa twitter, Trump aliandika jana kuwa amearifiwa na Urusi kuwa imewaondoa maafisa wake karibu wote kutoka Venezuela.

Lakini msemaji wa Ikulu ya Urusi Dmitry Peskov amesema hajui alichokimaanisha Trump, na kuongeza kuwa pengine kiongozi wa Marekani alikuwa akivinukuu vyanzo vya magazetini, kwa sababu Urusi haijatangaza kitu kama hicho.

Alisema maafisa wa Urusi wanaendelea kuwepo nchini Venezuela, wakizifanyia matengenezo zana za kijeshi zilizoko huko.

Mvutano umepanuka baina ya Marekani inayounga mkono kuangushwa kwa rais wa Venezuela Nicolas Maduro, na Urusi ambayo imeingilia kati kumkingia kifua kiongozi huo. Urusi imewapeleka maafisa wa jeshi wapatao 100 nchini Venezuela.