TIMU ya Simba inatarajia kucheza mchezo wa kirafiki Juni 21, mwaka huu dhidi ya timu ya Gwambina FC, ambapo Mchezo huo ambao utapigwa Uwanja wa Gwambina, Mwanza utatumika kama sehemu ya kutambulisha vifaa vyao vipya walivyosajili.



Simba ambao hadi sasa mchezaji wa nje ya timu yao waliomsajili ni Beno Kakolanya aliyetokea Yanga wanatarajiwa kufanya usajili kabambe ili kuendana na kasi ya michuano ya kimataifa.



Championi linafahamu kuwa Ibrahim Ajibu Ameshamaliza mkataba wake na Yanga na bado hajaongeza mwingine huku taarifa za chini zikisema kuwa ameshasaini mkataba wa awali na Simba na kuna uwezekano akaonekana kwenye mechi hiyo.



Akizungumza na Championi Jumatatu, Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara alisema kuwa wamealikwa kwenda kuzindua uwanja mpya wa Gwambina na wanafurahi kwa mwaliko huo ambapo wamepanga kutumia mchezo huo pia kutambulisha wachezaji wao wapya. “Tumealikwa kwenda kufungua Uwanja wa Gwambina uliopo Misungwi, Mwanza.



Ni heshima kubwa kwa Wanasimba wa Misungwi. Timu inatarajia kuondoka Juni 20 na mechi itapigwa Juni 21, wachezaji wapya wa ndani watachezea Simba kwa mara ya kwanza,” alisema Manara.