Tanzania inatarajia kupata Dola za Kimarekani milioni 75 (takribani Shilingi bilioni 172.5) kwa ajili ya kuboresha elimu ya ufundi stadi.

Fedha hizo zitatolewa na Benki ya Dunia (WB) kupitia mradi wake wa mafunzo ya ufundi kwa nchi za Afrika Mashariki (EASTRIP) utakaozinduliwa rasmi mwezi Juni, nchini Ethiopia.

Haya yamesemwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako alipozindua awamu ya kwanza ya programu ya Stadi za Ajira Tanzania (SET) , itakayoratibiwa na Shirika la Maendeleo na Ushirikiano la Uswisi (SDC).

Amesema mradi huo unashirikisha nchi tatu ikiwa ni pamoja na Kenya na Ethiopia na lengo kuu ni kuboresha mafunzo ya ufundi kwenye nchi zilizoteuliwa.

"Mradi huu utaunga mkono juhudi za serikali kuboresha elimu ya ufundi kwa Watanzania ili kufikia lengo la kuwa uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025,"aliongeza.