Tanzania imeongoza Afrika Mashariki kwa mujibu wa ripoti ya Global Peace Index (GPI) inayotolewa na taasisi ya uchumi na amani (IEP)yenye makao yake makuu mjini Sydney nchini Australia.

Tanzania imeshika nafasi ya 7 kwa kuwa nchi yenye amani kwa nchi za kusini mwa jangwa la Sahara na duniani ikiwa imeshuka kutoka nafasi ya 51 mwaka 2018 hadi nafasi ya 54 mwaka 2019 kati ya nchi 163, huku Iceland, New Zealand, Uholanzi, Austria, Denmark, Canada, Singapore, Slovenia, Japan, na Jamuhuri ya Czech ni nchi zilizoorodheshwa kuwa na amani zaidi duniani.

Wakati Tanzania ikiongoza Afrika Mashariki, Rwanda imeifuata ikiwa ya pili Afrika Mashariki lakini imeshika nafasi ya 17 kwa nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara, ikifuatiwa na Uganda iliyoshika nafasi ya 23 , Kenya ya nne Afrika Mashariki na 28 katika nchi za kusini mwa jangwa la Sahara.


Nchi zilizoshika nafasi za juu katika eneo la jangwa la sahara ni Mauritius, Botswana, Malawi, Ghana, Zambia na Sierre Leone.

Kwa mujibu wa Ripoti hiyo, nchi zilizo na kiwango cha chini cha amani ni Burundi,Chad, Cameroon, Mali, Nigeria, DR Congo, Somalia na Sudani Kusini.

Ripoti ya GPI inaonyesha kuwa dunia imekua na amani zaidi ikiwa ni kwa mara ya kwanza katika kipindi cha miaka mitano ikiwa imepanda kwa asilimia 0.09.

Ripoti hiyo inasema ongezeko la amani limetokana na kupungua kwa migogoro mikubwa duniani, hali iliyofanya kupungua kwa idadi ya vifo kutokana na migogoro ya ndani.